Mwanzo 7:1-24

  • Kuingia ndani ya safina (1-10)

  • Gharika duniani kote (11-24)

7  Baada ya hayo Yehova akamwambia Noa: “Ingia ndani ya safina, wewe pamoja na watu wote wa nyumbani mwako, kwa sababu nimekuona wewe peke yako kuwa mwadilifu mbele zangu miongoni mwa kizazi hiki.+  Ingia pamoja na wanyama safi wa kila aina, saba saba,*+ dume na jike; na wanyama wawili tu wasio safi wa kila aina, dume na jike;  pia viumbe wanaoruka angani saba saba,* dume na jike, ili kuhifadhi hai uzao wao duniani pote.+  Kwa maana baada ya siku saba tu, nitafanya mvua inyeshe+ duniani siku 40 mchana na usiku,+ nami nitafagilia mbali kutoka duniani kila kiumbe kilicho hai nilichokiumba.”+  Basi Noa akafanya yote ambayo Yehova alikuwa amemwamuru.  Noa alikuwa na umri wa miaka 600 maji ya gharika yalipokuja duniani.+  Kwa hiyo Noa, pamoja na wanawe, mke wake, na wake wa wanawe, wakaingia ndani ya safina kabla ya maji ya gharika kuja.+  Kila aina ya mnyama aliye safi na kila aina ya mnyama asiye safi na kila aina ya kiumbe anayeruka angani na kila aina ya kiumbe anayetambaa ardhini,+  wakaingia wawili wawili na kumjia Noa ndani ya safina, dume na jike, kama Mungu alivyokuwa amemwamuru Noa. 10  Na siku saba baadaye maji ya gharika yakaja duniani. 11  Katika mwaka wa 600 wa maisha ya Noa, mwezi wa pili, siku ya 17 ya mwezi huo, siku hiyo chemchemi zote za kilindi kikubwa cha maji zilifunguka kwa nguvu na malango ya mbinguni ya mafuriko yakafunguliwa.+ 12  Na mvua ikamwagika duniani kwa siku 40, mchana na usiku. 13  Siku hiyohiyo, Noa aliingia ndani ya safina pamoja na wanawe, Shemu, Hamu, na Yafethi,+ pamoja na mke wake na wake watatu wa wanawe.+ 14  Waliingia ndani pamoja na kila mnyama wa mwituni kulingana na aina yake, na kila mnyama wa kufugwa kulingana na aina yake, na kila mnyama anayetambaa duniani kulingana na aina yake, na kila kiumbe anayeruka kulingana na aina yake, kila ndege, kila kiumbe mwenye mabawa. 15  Waliendelea kumjia Noa ndani ya safina, wawili wawili, kila aina ya kiumbe mwenye pumzi ya uhai.* 16  Basi wakaingia ndani, dume na jike, viumbe wa kila aina, kama Mungu alivyokuwa amemwamuru. Baada ya hayo Yehova akaufunga mlango. 17  Gharika ikaendelea* kwa siku 40 duniani, na maji yakazidi kuongezeka, yakaanza kuibeba safina, nayo safina ikaelea juu sana duniani. 18  Maji yakafurika na kuzidi kuongezeka sana duniani, lakini safina ilielea juu ya maji. 19  Maji yalifurika sana duniani hivi kwamba milima yote mirefu chini ya mbingu ikafunikwa.+ 20  Maji yalipanda kufikia mikono 15* juu ya milima. 21  Basi viumbe wote walio hai waliotembea duniani wakafa+—viumbe wanaoruka, wanyama wa kufugwa, wanyama wa mwituni, viumbe wanaoishi katika makundi makubwa, na wanadamu wote.+ 22  Kila kiumbe katika nchi kavu aliyekuwa na pumzi ya uhai* katika mianzi ya pua yake akafa.+ 23  Basi Mungu akafagilia mbali kila kiumbe hai kutoka duniani, kutia ndani, wanadamu, wanyama, wanyama wanaotambaa, na viumbe wanaoruka angani. Wote walifagiliwa mbali kutoka duniani;+ ni Noa peke yake na wale waliokuwa pamoja naye ndani ya safina waliookoka.+ 24  Na maji yakaendelea kuifunika dunia kwa siku 150.+

Maelezo ya Chini

Au labda, “jozi saba za kila mnyama aliye safi.”
Au labda, “jozi saba za viumbe wanaoruka angani.”
Au “roho ya uhai.”
Au “ikaendelea kumwagika.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Au “pumzi ya roho ya uhai.”