Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naacha Jeshi Ili Nimtumikie Yehova

Naacha Jeshi Ili Nimtumikie Yehova

Naacha Jeshi Ili Nimtumikie Yehova

Limesimuliwa na Andrew Hogg

“Ikiwa wakati mmoja tutahitaji kutupa makombora yetu ya nyuklia,” akasema kamanda mkuu wa nyambizi yetu, “basi tutakuwa tumeshindwa kutimiza kusudi letu.” Maneno yake yalizua mazungumzo kuhusu ikiwa inafaa kujihusisha katika vita vya nyuklia. Lakini, nilianzaje kutumika katika nyambizi, kazi inayoitwa utumishi wa kimya kwa sababu tunajitahidi kubaki tukiwa tumejificha?

NILIZALIWA huko Philadelphia, Pennsylvania, Marekani, mwaka wa 1944. Nilipokuwa nikikua, baba yangu, babu yangu, na mjomba wangu ambao wote walikuwa wamewahi kutumikia jeshini, walinitia moyo nijiunge na jeshi kwa kuwa waliuona utumishi huo kuwa ndiyo kazi muhimu zaidi maishani. Nilipokuwa kijana, nilitembelea eneo la jeshi la majini na hapo ndipo nilipoona nyambizi kwa mara ya kwanza. Kuanzia wakati huo, nilijiwekea mradi wa kufanya kazi katika nyambizi. Nilipokuwa katika mwaka wangu wa mwisho katika shule ya sekondari, nilikubaliwa kuingia katika Chuo cha Marekani cha Jeshi la Wanamaji. Nilihitimu miaka minne baadaye, mnamo Juni (Mwezi wa 6) 1966.

Nilijiunga na Programu ya Jeshi la Wanamaji ya Kurusha Makombora ya Nyuklia ili nijifunze kuhusu mabomu ya nyuklia na kutumikia katika nyambizi. Kisha, Aprili (Mwezi wa 4) 1967, nilimwoa mke wangu mpendwa anayeitwa Mary Lee Carter. Mwishowe, mnamo Machi 1968, nilifikia mradi niliokuwa nimejiwekea nikiwa mtoto nilipotumwa kufanya kazi katika nyambizi inayoitwa USS Jack. Mwaka mmoja hivi baadaye, Mary Lee alijifungua mtoto wetu wa kwanza, binti yetu tuliyemwita Allison.

Mnamo 1971, niliwekwa kuwa Ofisa Mhandisi wa USS Andrew Jackson, ambaye kapteni wake alisema maneno yaliyotajwa mwanzoni mwa makala hii. Tulipokuwa baharini katika nyambizi hiyo ya kurusha makombora ya masafa marefu, tulikumbwa na moto, mkasa wenye kuogopesha zaidi kwa wafanyakazi wa nyambizi. Ulikuwa usiku wa manane, nami nilikuwa nikipumzika pamoja na maofisa wengine, tuliposikia kishindo. Kisha tukasikia king’ora kikilia, gong, gong, gong na tukasikia tangazo, “Moto katika chumba cha kwanza cha mitambo!”

Kwa kuwa nilikuwa msimamizi wa mitambo yote na mifumo ya umeme, nilikimbia ili nikaone tatizo lilikuwa nini. Moto ulikuwa umetokea katika jenereta moja ya kusambaza oksijeni katika nyambizi yetu. Mimi na wafanyakazi wengine watatu tulivalia mavazi fulani ya pekee na kuondoa gesi zozote ambazo zingeweza kuwaka. Hakuna yeyote aliyeumia. Licha ya mkasa huo, nyambizi yetu iliendelea kushika doria eneo iliyokuwa imegawiwa, hilo likionyesha kwamba wafanyakazi walikuwa wamezoezwa vizuri.

Niliamua Kusoma Kuhusu Mfanya Amani

Ili tuweze kukabiliana na hali ngumu za kazi, tulitiwa moyo tutenge saa kadhaa kila juma kusoma jambo fulani. Kwa kawaida nilisoma masimulizi ya maisha ya wanajeshi mashuhuri. Hata hivyo, pindi hiyo niliamua kusoma kumhusu mtu anayejulikana kuwa mfanya amani, yaani, Yesu Kristo. Nikitumia Biblia niliyopewa wakati wa kuhitimu kwangu katika chuo cha jeshi la wanamaji, nilianza kusoma vitabu vya Injili. Usomaji wangu ulizua maswali mengi. Nilihitaji msaada.

Tulipokuwa karibu kumaliza kushika doria, kamanda wetu mkuu alipanga kuwe na mkutano wa maofisa wa nyambizi yetu na akasema hivi: “Mhandisi wetu amepewa kazi bora zaidi katika Jeshi la Wanamaji la Marekani. Atakuwa Ofisa Mhandisi katika mojawapo ya nyambizi mpya zaidi za mashambulizi.” Nilipigwa na butwaa!

Mgawo wangu mpya ulifanya mimi na familia yangu tuhamie huko Newport News, Virginia, ambako nyambizi USS Los Angeles ilikuwa ikitengenezwa. Kazi yangu ilitia ndani kusimamia majaribio ya mitambo mbalimbali na kuandika miongozo ya kuendesha mitambo hiyo na programu za mafunzo. Kazi hiyo ilikuwa ngumu sana lakini iliniridhisha. Wakati huo, Mary Lee alijifungua mwana wetu, Drew. Sasa nilikuwa baba ya watoto wawili, na kwa mara nyingine nikaanza kuwaza kumhusu Mungu: ‘Ana maoni gani kuhusu vita? Ni nini hutupata tunapokufa? Je, kuna moto wa mateso?’

Mwishowe Napata Majibu!

Katika kipindi hicho mke wangu alianza kutembelewa na Mashahidi wa Yehova. Siku moja nilipopiga simu nyumbani, Mary Lee aliniambia hivi, “‘Wanawake wawili wa Biblia’ wamenitembelea.”

Nikauliza, “Wao ni wa dini gani?”

Akajibu, “Ni Mashahidi wa Yehova.”

Sikujua Mashahidi ni akina nani, lakini nilitaka kuielewa Biblia. Nikamwambia mke wangu, “Wakaribishe jioni moja.” Muda mfupi baada ya hapo, mmoja wao alirudi pamoja na mume wake, na mimi na mke wangu tukaanza kujifunza Biblia.

Mwishowe, nilianza kupata majibu ya maswali yaliyokuwa yamenitatanisha kwa miaka mingi. Kwa mfano, nilijifunza kwamba wafu “hawajui lolote kamwe,” ni kana kwamba wamelala usingizi mzito, ulinganisho ambao Yesu alitumia. (Mhubiri 9:5; Yohana 11:11-14) Kwa hiyo, wafu hawafurahii maisha au kuteseka mahali fulani lakini “wanalala” katika kifo, wakingojea kufufuliwa.

Pia, mimi na Mary Lee tulianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo katika Jumba la Ufalme. Tuliona Mashahidi—kutoka tamaduni, viwango vya elimu, na mataifa mbalimbali—wote wakimtumikia Mungu kwa amani na umoja. Mimi na mke wangu tulikata kauli kwamba “kwa kweli Biblia inaweza kubadili maisha ya watu.”—Zaburi 19:7-10.

Wakati wa Kufanya Uamuzi

Vita vya Waarabu na Waisraeli vilipozuka katika mwaka wa 1973, nyambizi za Marekani zilizoshika doria katika Bahari ya Atlantiki zilitumwa vitani. Mambo yangekuwa mabaya, na wakati huo nikaanza kutambua kwamba ni Ufalme wa Mungu tu, na si siasa za wanadamu, utakaoleta amani ya kweli na ya kudumu. Kwa kweli, mara nyingi nilikuwa nimesali “Ufalme wako uje, Mapenzi yako na yatimizwe, hapa duniani,” lakini sikujua maneno hayo yanamaanisha nini. (Mathayo 6:9, 10, Union Version) Hata hivyo, sasa nilielewa kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali ya kimbingu ambayo hivi karibuni itatawala juu ya dunia yote, na kuondoa uovu wote pamoja na watenda maovu.—Danieli 2:44; 7:13, 14.

Andiko ambalo hasa lilinisumbua lilikuwa 2 Wakorintho 10:3, 4. Linasema kwamba Wakristo wa kweli ‘hawapigi vita kulingana na walivyo katika mwili. Kwa maana silaha za vita vyao si za kimwili, bali ni zenye nguvu kwa Mungu.’ Nilijifunza kwamba “silaha” hizo ni za kiroho, na zinatia ndani “upanga wa roho,” yaani, Biblia Takatifu.—Waefeso 6:17.

Sasa nilikuwa nimefika kwenye njia panda. Je, ningeendelea kufanya kazi yangu ya kijeshi, ambayo niliifurahia licha ya changamoto zake, au ningepatanisha maisha yangu na kweli za Biblia? Baada ya kusali kuhusu jambo hilo, nilikata kauli kwamba ikiwa kweli ningependa kuwa mfanya amani, ninapaswa kuifanya kama Mungu anavyotaka.

Napata “Amiri-Jeshi Mkuu” Mpya

Mimi na Mary Lee tulisali na kuzungumza kuhusu wakati wetu ujao na tukaazimia kwamba tutamtumikia “Amiri-Jeshi Mkuu”—Yehova Mungu. Sote tuliamua kujiweka wakfu kwa Yehova na nikaandika barua ya kujiuzulu kutoka kwenye jeshi la wanamaji. Nilihamishwa na kupelekwa huko Norfolk, Virginia, ili nisubiri ruhusa ya kuondoka. Wengi kati ya maofisa wenzangu walishangazwa na uamuzi wangu, na hata wengine walinipinga vikali. Lakini wengine walipendezwa na msimamo wangu uliotegemea Biblia na wakaheshimu uamuzi wangu.

Niliruhusiwa kuondoka mnamo 1974. Mwaka huohuo mimi na mke wangu tulionyesha wakfu wetu kwa kubatizwa katika Kusanyiko la Wilaya la “Divine Purpose” la Mashahidi wa Yehova huko Hampton, Virginia. (Mathayo 28:19, 20) Maisha yetu mapya yalikuwa yameanza.

Kukabiliana na Vipingamizi Vipya

Mimi na Mary Lee tulikuwa na watoto wawili wachanga, hatukuwa na kazi, na tulikuwa tu na pesa ambazo zingetusaidia kwa miezi michache. Nilituma maombi ya kazi kwa waajiri kadhaa na nikaacha jambo hilo mikononi mwa Mungu. Baada ya muda mfupi, kampuni fulani iliniajiri. Mshahara ulikuwa nusu ya ule niliokuwa nikilipwa jeshini, lakini kazi hiyo ilitutimizia mahitaji yetu.

Mimi na mke wangu tulipofanya maendeleo ya kiroho, tulitaka kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova. Familia moja ya Mashahidi ambayo tulijua, ilikuwa imehamia katika eneo la Virginia ya kati ambako kulikuwa na uhitaji wa walimu wa Biblia, na walitualika tuwatembelee. Tulitembea huko mara moja tu nasi tukaanza kufanya mipango ili tuhamie huko. Niliomba nihamishwe kazini, na nilifurahi sana ombi langu lilipokubaliwa. Na hata nilipandishwa cheo! Isitoshe, kampuni hiyo ilikubali kulipia gharama za kuhama. Tulijiambia hivi, ‘Kwa kweli Mungu huwajali wale wanaojitahidi kufanya mapenzi yake.’—Mathayo 6:33.

Kwa kuwa familia yetu imekuwa ikiishi maisha rahisi, mimi na Mary Lee tumetumikia tukiwa watumishi wa wakati wote. Kufanya hivyo kulituwezesha kutumia wakati mwingi pamoja na watoto wetu wawili walipokuwa wakikua. Kwa kweli, kufanya hivyo kumetuletea shangwe isiyo na kifani, kwa kuwa Allison na Drew wanaendelea “kutembea katika kweli.”—3 Yohana 4; Methali 23:24.

Naam, pindi fulani matatizo ya kiuchumi, kodi ya nyumba, matatizo ya afya, na matatizo ya uzeeni yametufanya tuwe na wasiwasi. Lakini sikuzote Yehova ametutegemeza. Je, ninaghairi kwamba niliacha kazi ya jeshi? La hasha! Tunapotafakari kuhusu maisha yetu, mimi na Mary Lee tunaweza kusema bila shaka yoyote kwamba kumtumikia Yehova ndiyo kazi muhimu zaidi maishani na yenye kuthawabisha.—Mhubiri 12:13.

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Tuliazimia kumtumikia “Amiri-Jeshi Mkuu”

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Nyambizi USS “Los Angeles”

[Hisani]

U.S. Navy photo

[Picha katika ukurasa wa 13]

Picha ya karibuni ya mimi na Mary Lee