Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nivae Nini?

Nivae Nini?

Vijana Huuliza

Nivae Nini?

Heather anajitayarisha kuondoka, na wazazi wake hawaamini macho yao. “Unaenda wapi ukiwa umevaa hivyo?” baba yake anauliza. “Ninaenda madukani pamoja na rafiki zangu. Kwani nguo niliyovaa ina ubaya gani?” Heather anauliza kwa mshangao. “Huendi popote ukiwa umevaa hivyo!” mama yake anamwambia. “Lakini Mama,” Heather analalamika, “watoto wote wanavaa hivi siku hizi. . . . Huu ndio mtindo mpya!” “Lakini sisi hatutaki mtindo huo hapa!” Baba yake anamjibu kwa ukali. “Nenda ukabadili nguo hizo mara moja, la sivyo huendi popote!”

MIZOZO kuhusu mavazi haikuanza leo. Huenda wazazi wako walipokuwa vijana walizozana vivyo hivyo na wazazi wao. Na huenda wao walihisi kama unavyohisi leo! Lakini sasa wao ndio wazazi, na suala la ni nini utakachovaa linaibua kasheshe moja baada ya nyingine.

Wewe unasema: Vazi hili ni zuri.

Wao wanasema: Ni shaghala-baghala.

Wewe unasema: Linavutia sana.

Wao wanasema: Linawavutia watu kingono.

Wewe unasema: Bei yake ni nusu ile ya kawaida.

Wao wanasema: Kwa sababu linafunika nusu tu ya sehemu inayopaswa kufunika!

Je, kuna njia yoyote ya kusuluhisha mzozo huo? Ndiyo! Megan, ambaye sasa ana umri wa miaka 23 anajua jinsi ya kuusuluhisha. “Hakuna haja ya kubishana,” anasema. “Mnaweza kupatana.” Eti kupatana? Je, hilo linamaanisha uvae kama mtu aliye na umri wa miaka 40? Tulia! Kupatana kunamaanisha kwamba wewe na wazazi wako mzungumzie tofauti zenu na kutafuta suluhisho ambalo linawafurahisha wao—na wewe pia. Hilo lina faida gani?

1. Utapendeza, hata mbele ya rafiki zako.

2. Wazazi wako hawatachambua sana unachovaa.

3. Baada ya kuona jinsi unavyovaa, huenda wazazi wako wakakupa uhuru zaidi.

Hebu fikiria vazi fulani ambalo umeona kwenye Intaneti au kwenye duka na unaona ni lazima uwe nalo. Jambo la kwanza unalopaswa kufanya ni . . .

Fikiria Kanuni za Biblia

Biblia haisemi mengi kuhusu mavazi. Kwa kweli, unaweza kusoma kwa sauti Maandiko yote yanayozungumzia jambo hilo kwa dakika chache tu! Hata hivyo, bado utapata mwongozo unaofaa. Kwa mfano:

▪ Biblia inawashauri wanawake wajipambe kwa “kiasi na utimamu wa akili.” *1 Timotheo 2:9, 10.

Huenda neno “kiasi” likakutia wasiwasi. ‘Je, hiyo inamaanisha nivae gunia?’ huenda ukajiuliza. La hasha! Katika muktadha huu, kuwa na kiasi kunamaanisha uvae nguo zinazoonyesha kwamba unajiheshimu na unajali hisia za wengine. (2 Wakorintho 6:3) Kuna nguo nyingi sana zinazoweza kuonyesha kwamba una kiasi. Danielle, mwenye umri wa miaka 23 anasema, “Huenda ikawa vigumu kupata nguo zenye kiasi lakini unaweza kuvaa mavazi ya kisasa yasiyopita kiasi.”

▪ Biblia inasema kwamba badala ya kukazia sura ya nje, unapaswa kukazia “mtu wa siri wa moyoni.”—1 Petro 3:4.

Vazi lisilo na kiasi linaweza kuwavutia watu kwa muda, lakini urembo wa ndani ndio utakaowafanya watu wazima na rafiki zako wakuheshimu kwa muda mrefu. Eti hata rafiki zako? Ndiyo—hata wao wanaweza kuona upumbavu wa kuvaa mavazi yenye mtindo unaopita kiasi. “Inakera sana kuona jinsi wanawake wanavyojianika mbele za wanaume kwa mavazi wanayovaa!” anasema Brittany mwenye umri wa miaka 16. Kay anakubaliana naye. Akieleza jinsi rafiki yake wa zamani alivyokuwa akivaa, anasema: “Kila kitu alichokuwa akivaa kilikusudia tu kuwavutia wanaume. Alitaka wavutiwe naye kwa hiyo alivaa mavazi yanayovuta fikira za watu.”

Dokezo: Epuka mavazi yatakayowavutia watu kingono. Yanawafanya watu wafikiri unataka sana mtu wa jinsia tofauti au unajifikiria tu. Pia yanaweza kufanya uchokozwe, au utendewe jambo baya. Tofauti na hilo, mavazi yenye kiasi yanaboresha jinsi unavyoonekana na kukazia sifa zako nzuri.

Waombe Wazazi Wako Maoni

Kuficha vazi lisilofaa katika mkoba wako unapoondoka nyumbani na kisha kulivaa baadaye si jambo linalofaa. Wazazi wako watakuamini zaidi ikiwa utakuwa mnyoofu na kusema mambo waziwazi, hata kuhusiana na mambo ambayo unafikiri unaweza kufanya bila wao kujua. Kwa kweli, huenda ikafaa uwaombe maoni unapochagua mavazi.—Methali 15:22.

Lakini kwa nini uwaombe maoni? Si wazazi wako watakukataza kuvaa mavazi ya kisasa? Sivyo hata kidogo. Ni kweli kwamba huenda wazazi wako wakawa na maoni tofauti na yako. Lakini nyakati nyingine hilo ndilo unalohitaji. Nataleine mwenye umri wa miaka 17 anasema, “Ninathamini sana mashauri ya wazazi wangu, kwa sababu sitaki kutoka nje na kujiaibisha au kuwafanya watu waniseme vibaya kwa sababu ya mavazi yangu.”

Isitoshe, kumbuka jambo hili: Ikiwa bado unaishi na wazazi, basi uko chini ya mamlaka yao. (Wakolosai 3:20) Hata hivyo, ukielewa maoni yao, nao waelewe yako, utashangaa kwamba mtakubaliana mara nyingi. Kwa sababu hiyo, huenda mkaacha kuzozana kuhusu mavazi!

Dokezo: Unapojaribu nguo fulani, fikiria mambo zaidi ya yale unayoona kwenye kioo. Vazi linaloonekana kuwa lenye kiasi huenda lisiwe hivyo unapoketi au kuinama kuokota kitu. Ikiwezekana, omba maoni kutoka kwa wazazi wako au rafiki mkomavu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Ingawa mashauri kama hayo ya Biblia yameelekezwa kwa wanawake, kanuni hizo zinawahusu wanaume pia. Ona sanduku  “Namna Gani Wavulana?”

MAMBO YA KUFIKIRIA

Fikiria vazi ambalo ungependa kununua. Kisha ujiulize hivi:

▪ Vazi hilo linawapa watu “ujumbe” gani?

▪ Watu watakuwa na maoni gani wakiniona nimevalia hivi?

▪ Je, kweli ninataka watu wawe na maoni hayo na matokeo yatakuwa nini?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]

Chati ya Kukusaidia Kununua Mavazi

Maagizo: Toa nakala ya ukurasa huu. Wape wazazi wako wajaze safu kwenye upande wa kulia nawe ujaze safu ya upande wa kushoto. Baada ya kufanya hivyo, badilishaneni chati hizo na mzungumzie majibu yenu. Je, kuna majibu yanayowashangaza? Ni jambo gani jipya ambalo kila mmoja wenu amejifunza kuhusu maoni ya mwenzake?

UPANDE WAKO

Fikiria kuhusu nguo ambayo ungependa kuvaa au kununua.

▪ Kwa nini unapenda nguo hiyo? Andika namba kando ya sababu zilizoandikwa hapa chini, ukianza na ile ambayo ukianza na ile ambayo ungetanguliza.

․․․․․ Jina la watengenezaji

․․․․․ Inawavutia watu wa jinsia tofauti

․․․․․ Vijana wenzangu wanaipenda

․․․․․ Inastarehesha

․․․․․ Ni ya bei nafuu

․․․․․ Sababu nyingine ․․․․․

▪ Huenda wazazi wangu’ watasema hivi kuhusu nguo hii

“Usiinunue!”

“Labda unaweza.”

“Ni sawa.”

▪ Huenda wakakataa kwa sababu

“Inawavutia watu kingono.”

“Inakufanya uonekane shaghala-baghala.”

“Mtindo wake umepita kiasi.”

“Inatuletea sifa mbaya tukiwa wazazi wako.”

“Ni bei ghali sana.”

Sababu nyingine ․․․․․

TUNAWEZA KUPATANAJE?

▪ Maoni ya wazazi wangu yananisaidiaje?

․․․․․

▪ Je, nguo hii inaweza kurekebishwa, ili ifae?

․․․․․

UPANDE WA WAZAZI WAKO

Fikiria kuhusu nguo ambayo kijana wako angependa kuvaa au kununua.

▪ Unafikiri ni kwa nini anapenda nguo hiyo? Andika namba kando ya sababu zilizoandikwa hapa chini, ukianza na ile ambayo unafikiri angetanguliza.

․․․․․ Jina la watengenezaji

․․․․․ Inawavutia watu wa jinsia tofauti

․․․․․ Vijana wenzangu wanaipenda

․․․․․ Inastarehesha

․․․․․ Ni ya bei nafuu

․․․․․ Sababu nyingine ․․․․․

 ▪ Huenda nikasema hivi kuhusu nguo hii

“Usiinunue!”

“Labda unaweza.”

“Ni sawa.”

▪ Sababu yangu ya kukataa ni

“Inawavutia watu kingono.”

“Inakufanya uonekane shaghala-baghala.”

“Mtindo wake umepita kiasi.”

“Inatuletea sifa mbaya tukiwa wazazi wako.”

“Ni bei ghali sana.”

Sababu nyingine ․․․․․

TUNAWEZA KUPATANAJE?

▪ Je, tunakataa nguo hii kwa sababu tu ya mapendezi yetu?

Ndiyo Labda Hapana

▪ Je, nguo hii inaweza kurekebishwa, ili ifae??

․․․․․

UAMUZI

․․․․․

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Ni sawa kuvalia mitindo ya kisasa, maadamu haipingani na kanuni za Biblia. Kuna mavazi mengi unayoweza kununua ambayo ni mazuri na yanafaa.”—Derrick.

“Nilipokuwa tineja, nilitaka kuwa na uhuru zaidi. Sikupenda kuambiwa nivae nini. Hata hivyo, baada ya muda nilitambua kwamba sikuwa nikiheshimiwa kama nilivyotaka—hadi nilipoanza kusikiliza maoni ya wazazi wangu na watu wenye umri mkubwa.”—Megan.

“Ninapowaona wasichana wakivaa mavazi yenye kuwavutia watu kingono, mimi huacha kuwaheshimu. Kwa upande ule mwingine, ninapowaona watu wakiwa wamevaa mavazi yenye kiasi lakini yanayovutia, mimi hujiambia, ‘Hivyo ndivyo ninavyotaka watu wanione.’”—Nataleine.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

NAMNA GANI WAVULANA?

Kanuni za Biblia zilizozungumziwa katika makala hii zinawahusu wavulana pia. Uwe mwenye kiasi. Acha watu waone yule mtu wa siri wa moyoni, yaani, sifa zako za ndani. Unapofikiria kuvaa kwa njia fulani, jiulize: ‘Mavazi haya yanaonyesha nini kunihusu? Je, yanaonyesha jinsi nilivyo kikweli?’ Kumbuka, mavazi yanakutambulisha. Hakikisha kwamba mavazi yako yanawakilisha kanuni unazofuata!

[Sanduku katika ukurasa wa 21]

TAARIFA KWA WAZAZI

Fikiria mfano ulio mwanzoni mwa makala hii, na uwazie kwamba Heather ni binti yako. Umeona kwamba vazi alilovaa linaonyesha sana sehemu za mwili, kwa maoni yako ni kana kwamba hakuna kitu kimefichwa. Unasema mara moja, “Nenda ukabadili nguo hizo mara moja, la sivyo huendi popote!” Bila shaka, atabadili vazi hilo mara moja kwa sababu hana la kufanya. Lakini unawezaje kumfanya abadili kufikiri kwake na si mavazi yake tu?

▪ Kwanza, kumbuka kwamba lazima kijana wako atambue matokeo ya kuvaa kwa njia isiyo na kiasi kama wewe unavyoyatambua. Kwa kweli, kijana wako hataki kuonekana kama mjinga au kuvuta uangalifu wa watu kwa njia isiyofaa. Mweleze kwa subira kwamba nguo zisizo na kiasi hazivutii. * Mpendekezee mavazi mengine.

▪ Pili, “usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5) Jiulize, ‘Je, vazi hilo linavunja kanuni ya Biblia, au ni kwamba silipendi tu?’ (2 Wakorintho 1:24) Ikiwa ni mapendezi yako tu, je, unaweza kumruhusu kijana wako alivae?

▪ Tatu, usimwambie tu kijana wako kwamba vazi lake halifai. Msaidie kutafuta mavazi yanayofaa. Wakati unaotumia na jitihada zako hazitakuwa za bure.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 101 Kijana wako anayebalehe anahangaikia sana jinsi mwili wake ulivyo, kwa hiyo, uwe mwangalifu usiseme au kudokeza kwamba ana kasoro.