Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Teknolojia—Fikiria Wengine na Gharama

Teknolojia—Fikiria Wengine na Gharama

Teknolojia—Fikiria Wengine na Gharama

Katherine, ambaye ana umri wa miaka 20 na kitu, hutumia kompyuta kazini. Lakini akiwa nyumbani, yeye hujipata akitumia Intaneti kutafuta habari, kununua vitu, na kuwasiliana kupitia barua-pepe. Hata hivyo, yeye hatumii teknolojia sana akilinganishwa na wafanyakazi wenzake wenye umri mdogo. “Kwa nini wananisumbua kwa kunitumia ujumbe wa kijinga kila mara?” anauliza. “Si mimi ni mwanadamu! Mbona wasizungumze nami kwenye simu?”

SWALI hilo la Katherine linachekesha kwa kuwa mtu anapotumia simu bado hawasiliani na mwenzake uso kwa uso. Hata hivyo, hoja ya Katherine ina msingi: Huenda vifaa vingi vya teknolojia ambavyo vimekusudiwa kuwaunganisha watu, vikawatenganisha kihisia. Ili uwe na usawaziko unapotumia teknolojia, fikiria kanuni zifuatazo za Biblia.

“Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Tukifuata maneno hayo ya Yesu Kristo tunapotumia simu za mkononi na kompyuta, tutawatendea wengine kwa heshima na kuwa na adabu. Mwanamke mmoja anayeitwa Anne anasema hivi: “Mimi na mume wangu tulikuwa katika mkahawa mmoja. Wanaume wawili walikuwa wakila chakula meza iliyokuwa kando yetu. Hata hivyo, mmoja wao alitumia muda wote akizungumza kwenye simu na kula. Tulimhurumia sana mwenzake, ambaye ni kana kwamba alikuwa akila peke yake.” Ungehisije ikiwa ungekuwa pamoja na mwanamume huyo? Ungeumia? Au ungeudhika? Hata kama tunaweza kutumia simu zetu za mkononi mahali popote, wakati wowote, haimaanishi kwamba tufanye hivyo. Kanuni iliyo katika maneno ya Yesu inapaswa kutuongoza.

“Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa.” (Waefeso 5:15, 16) Wakati ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu na haupaswi kupotezwa. Ni kweli kwamba teknolojia inaweza kuokoa wakati. Kwa mfano, mtu anaweza kufanya utafiti, shughuli za benki, na kununua vitu haraka akitumia Intaneti. Lakini pia anaweza kupoteza muda mwingi akirandaranda kwenye Intaneti bila kusudi lolote.

Pia mtu anaweza kupoteza wakati mwingi akijaribu kufanya mambo kadhaa kwa wakati mmoja, kama vile, kutumia kompyuta huku ukitazama televisheni, kuzungumza kwenye simu, au kujaribu kutuma barua-pepe huku ukijaribu kufungua programu nyingine za kompyuta. Kwa nini kufanya mambo kadhaa kwa wakati mmoja hakuleti matokeo mazuri?

Dakt. Jordan Grafman mtaalamu wa mfumo wa neva anasema kwamba “mtu hawezi kupata ujuzi mwingi wa kazi yoyote anapojaribu kufanya mambo kadhaa kwa wakati mmoja.” Hatuwezi kukazia fikira mambo kadhaa wakati uleule; kuna jambo fulani ambalo hatutafanya vizuri. Tunapojaribu kufanya mambo kadhaa kwa wakati mmoja huenda tukayafanya kijuujuu tu na hatutayakumbuka vizuri. Pia, kufanya jambo moja na kisha kubadilika haraka kufanya lingine, huwafanya watu wakosee mara nyingi zaidi na “kunachukua muda mrefu zaidi—huenda hata mara mbili au zaidi ya wakati ambao wangetumia ikiwa wangefanya kazi hizo kwa mpango,” inasema ripoti fulani katika gazeti Time. Kwa hiyo, usifanye mambo kadhaa kwa wakati mmoja; huenda usitimize mambo ambayo ulitaka kutimiza!

“Mjilinde na kila namna ya tamaa, kwa sababu hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Vitu vya kimwili hata viwe vya gharama au vya kifahari namna gani haviwezi kumpa mtu uhai au furaha ya kweli. Ni Mungu peke yake anayeweza kufanya hivyo. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Kwa upande ule mwingine, ulimwengu wa kibiashara unasema kwamba furaha ya kweli inatokana na vitu vya kimwili. ‘Nunua, nunua, nunua,’ ndivyo ulimwengu huo unavyosema. ‘Unapaswa kuwa na vitu vya kisasa zaidi.’ Usidanganyike. Badala yake, uwe na hekima. Kabla ya kutumia pesa, chunguza nia yako ni nini na kama unahitaji kitu fulani. Kumbuka pia kwamba vifaa vingi vya hali ya juu hupoteza thamani upesi sana. Kwa hiyo, ikiwa unahitaji kifaa fulani, jiulize hivi: ‘Je, ni lazima niwe na kifaa cha kisasa zaidi? Na je, ninahitaji kifaa kilicho na mambo ya ziada yanayogharimu sana, ambayo huenda sitawahi kuyatumia?’

Baraka au Laana—Uamuzi Ni Wako

Katherine, aliyetajwa awali, alipatwa na wasiwasi mwingi kompyuta yake ya nyumbani ilipoharibika. “Mwanzoni nilipatwa na mshtuko,” anasema, “lakini nikaamua sitanunua nyingine haraka. Baada ya mwezi mmoja, nilitulia na nikapata muda mwingi wa kusoma. Ninatumia kompyuta kazini, kwa hiyo ninaweza kuendelea kuwasiliana na rafiki zangu baada ya kazi. Lakini sihisi tena ni kana kwamba ninahitaji kupata habari kila wakati. Teknolojia haiongozi maisha yangu tena.”

Kwa kweli, vifaa vingi vya sayansi na teknolojia vinafaa na vinaweza kuokoa wakati na nguvu zetu nyingi. Vitumie ikiwa tu ni lazima, lakini ufanye hivyo kwa hekima na kwa kuwafikiria wengine. Jinsi gani? Watangulize wanadamu wenzako badala ya kutanguliza teknolojia. Usipoteze wakati na pesa kwa kununua vifaa au programu za kompyuta usizohitaji. Usitumie Intaneti na vifaa vingine kutazama picha chafu na jeuri. Na usiwe “mraibu” wa teknolojia. Kwa ufupi, uwe na hekima—tumia kanuni ambazo zimethibitika kuwa zinafaa, zilizoongozwa na roho ya Mungu ambazo zinapatikana katika Biblia Takatifu, Neno la Mungu lililoandikwa. Naam, “Yehova mwenyewe anatoa hekima; kinywani mwake hutoka ujuzi na utambuzi.”—Methali 2:6.

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

KUTUMIA SIMU NA KOMPYUTA KWA ADABU

Unaweza kutumiaje simu ya mkononi na kompyuta kwa njia inayoonyesha kwamba unawajali wengine? Fikiria mambo yafuatayo.

▪ Epuka kupiga au kupokea simu wakati na mahali ambapo utawasumbua wengine. Ikiwezekana, zima simu yako.

▪ Ikiwa unazungumza na mtu ana kwa ana, usiruhusu simu ikatize mazungumzo hayo isipokuwa iwe lazima kufanya hivyo.

▪ Unapozungumza kwenye simu, mkazie fikira yule unayezungumza naye.

▪ Usimpige mtu picha kwa kutumia simu yako ya mkononi ikiwa utamkosea heshima au utamwaibisha kwa kufanya hivyo.

▪ Epuka kishawishi cha kuwatumia watu barua-pepe yoyote unayopata hata ingawa huenda ikaonekana kuwa yenye kupendeza sana. Huenda wale unaowatumia wasifurahie kuipokea.