Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nizungumze Jinsi Gani na Wazazi Wangu?

Nizungumze Jinsi Gani na Wazazi Wangu?

Vijana Huuliza

Nizungumze Jinsi Gani na Wazazi Wangu?

“Nilijaribu sana kuwaambia wazazi wangu jinsi nilivyohisi, lakini sikuweza kujieleza vizuri, nao walinikatiza mara moja. Ingawa ilichukua ujasiri mwingi kuwaeleza tatizo langu, sikufaulu!”—Rosa. *

ULIPOKUWA mchanga, huenda hukuogopa kuwaomba wazazi wako mashauri. Uliwaambia kila kitu, mambo ya maana na hata yale yasiyo ya maana. Ulijieleza kwa uhuru na uliamini kila kitu walichokuambia.

Hata hivyo, sasa huenda unahisi kwamba wazazi wako hawakuelewi hata kidogo. “Jioni moja wakati wa mlo nilianza kulia na kuwaeleza wazazi hisia zangu,” anasema msichana anayeitwa Edie. “Walinisikiliza, lakini ni kana kwamba hawakunielewa.” Matokeo yalikuwaje? “Nilienda chumbani mwangu na kulia zaidi!”

Kwa upande ule mwingine, nyakati nyingine huenda ukaamua kutowaeleza wazazi wako hisia zako. “Mimi huzungumza na wazazi wangu kuhusu mambo mengi sana,” anasema mvulana anayeitwa Christopher. “Lakini nyakati nyingine mimi hupenda wasijue kila kitu ninachofikiria.”

Je, ni vibaya kuficha mambo fulani? Si vibaya, maadamu hufanyi hivyo kwa hila. (Methali 3:32) Hata hivyo, iwe wazazi wako hawakuelewi au wewe huwaelezi kila kitu, jambo moja ni muhimu sana: Unahitaji kuzungumza na wazazi wako—nao wanahitaji kukusikia ukijieleza.

Endelea Kuzungumza!

Kwa njia fulani, kuwasiliana na wazazi wako ni kama kuendesha gari. Unapopata kizuizi barabarani, huachi kuendesha gari; unatafuta tu njia nyingine. Fikiria mifano kadhaa.

Kizuizi cha 1: Unataka kuzungumza, lakini ni kana kwamba wazazi wako hawakusikilizi. “Ni vigumu kwangu kuzungumza na baba yangu,” anasema Leah. “Nyakati nyingine ninaweza kuzungumza naye kwa muda kisha aniambie, ‘Pole, ulikuwa ukizungumza na mimi?’”

SWALI: Vipi ikiwa Leah anahitaji sana kuzungumzia tatizo lake? Anaweza kutumia njia tatu.

Njia A

Kumfokea baba yake. Leah anaweza kupaaza sauti na kusema: “Ninakuambia jambo muhimu! Sikiliza!”

Njia B

Kuacha kuzungumza na baba yake. Leah anaweza kuacha kabisa kuzungumza na wazazi wake kuhusu matatizo yake..

Njia C

Kusubiri hadi wakati mwingine unaofaa na kuzungumzia tatizo lake. Leah anaweza kuzungumza moja kwa moja na baba yake, au anaweza hata kumwandikia barua kuhusu tatizo lake.

Wewe unafikiri Leah anapaswa kutumia njia gani? ․․․․․

Acheni tuchunguze njia zote tuone zitakuwa na matokeo gani. Baba ya Leah amekengeushwa na mambo mengine, kwa hiyo hatambui kwamba Leah amevunjika moyo. Kwa hiyo, ikiwa Leah atachagua Njia A, baba yake hataelewa kwa nini anamfokea. Huenda bado baba yake asimsikilize, na kufanya hivyo huenda kusionyeshe kwamba anawaheshimu wazazi wake. (Waefeso 6:2) Kwa hiyo, kufanya hivyo hakuleti manufaa.

Ingawa huenda ikawa rahisi kutumia Njia B, huenda kufanya hivyo kusiwe jambo la hekima. Kwa nini? Kwa sababu “mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri, lakini katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.” (Methali 15:22) Ili ashughulikie matatizo yake kwa mafanikio, Leah anahitaji kuzungumza na wazazi wake, na ili wamsaidie, wanahitaji kujua mambo yanayoendelea maishani mwake. Kukataa kuzungumza hakuwezi kumsaidia.

Hata hivyo, akitumia Njia C Leah hataruhusu kizuizi kimzuie. Badala yake, anajaribu kuzungumzia jambo hilo wakati mwingine. Na akiamua kumwandikia baba yake barua, huenda Leah akatulia mara moja. Kuandika barua hiyo kunaweza pia kumsaidia kuchagua maneno hususa atakayotumia wakati baba yake anasikiliza. Anaposoma barua hiyo, baba ya Leah ataelewa kile anachoambiwa, na hilo litamsaidia kumwelewa Leah vizuri zaidi. Njia C inamnufaisha Leah na baba yake.

Leah angetumia njia gani nyingine? Andika njia hizo hapa chini. Kisha uandike ni matokeo gani yangepatikana kwa kutumia njia hiyo.

․․․․․

Kizuizi cha 2: Wazazi wako wanataka kuzungumza nawe, lakini wewe hutaki. “Hakuna kitu kinachoudhi kama kuulizwa maswali mengi baada ya kutoka shuleni na kufika nyumbani ukiwa umechoka,” anasema msichana anayeitwa Sarah. “Mimi hutaka kusahau mambo yote yaliyotokea shuleni, lakini mara moja wazazi wangu huanza kuuliza: ‘Siku ilikuwaje? Ulipata matatizo yoyote?’” Bila shaka, wazazi wa Sarah huuliza maswali hayo wakiwa na nia nzuri. Lakini bado yeye anasema, “Ni vigumu kuzungumza kuhusu mambo ya shule nikiwa nimechoka na kufadhaika.”

SWALI: Sarah anaweza kufanya nini akiwa chini ya hali kama hiyo? Kama mfano uliotangulia ulivyoonyesha, anaweza kutumia njia tatu.

Njia A

Kukataa kuzungumza. Anaweza kusema: “Achaneni na mimi. Sitaki kuzungumza sasa hivi!”

Njia B

Kuzungumza. Licha ya kuhisi, Sarah anaweza kujibu maswali ya wazazi wake akiwa amenuna.

Njia C

Aahirishe kuzungumza kuhusu shule hadi wakati mwingine lakini aendelee kuzungumzia jambo lingine. Sarah anaweza kupendekeza kwamba wazungumze kuhusu shule wakati mwingine, akili yake itakapokuwa imetulia zaidi. Kisha anaweza kuuliza hivi kwa unyoofu: “Siku yako ilikuwaje?”

Wewe unafikiri Sarah anapaswa kutumia njia gani? ․․․․․

Acheni tuchunguze tena njia zote tuone zitakuwa na matokeo gani.

Kabla ya kuchagua Njia A, Sarah anahisi amefadhaika na hataki kuzungumza. Akichagua kutumia njia hii, bado hatajihisi vizuri na hata atajihisi akiwa na hatia kwa kuwafokea wazazi wake.—Methali 29:11.

Wakati huohuo, huenda wazazi wa Sarah wakakasirishwa kwa kuwa Sarah amewafokea—na pia huenda wasifurahishwe na kunyamaza kwake. Wanaweza kufikiri kwamba Sarah anawaficha jambo fulani. Wanaweza hata kujaribu kumchimba kwa maneno, na bila shaka kufanya hivyo kutamkasirisha Sarah hata zaidi. Hatimaye, kutumia njia hii hakuleti manufaa.

Njia B ni afadhali kuliko Njia A. Bado Sarah na wazazi wake watakuwa wakiongea. Lakini kwa kuwa mazungumzo yao hayatakuwa ya kutoka moyoni, Sarah na wazazi wake hawatapata kile wanachotaka, yaani, mazungumzo matulivu na ya wazi.

Hata hivyo, ikiwa atatumia Njia C, Sarah atajihisi vizuri kwa sababu mambo ya shule hayajazungumziwa. Wazazi wake watafurahi kwa kuwa anataka kuzungumza nao. Huenda hii ikawa ndiyo njia bora kwani wote wanatumia kanuni inayopatikana kwenye Wafilipi 2:4, inayosema: ‘Mtu asitafute faida yake mwenyewe tu bali faida ya mwenzake.’—Biblia Habari Njema.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Kuna uhusiano gani kati ya kuchagua wakati unaofaa na kuwasiliana?—Methali 25:11.

▪ Kwa nini inafaa ujitahidi kuzungumza na wazazi wako?—Ayubu 12:12.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]

NJIA NYINGINE

Je, Yale Unayosema Yanaeleweka Vibaya? Je, unashindwa kuwasiliana na wazazi wako? Huenda maneno yako yanawasilisha ujumbe tofauti.

Unaposema . . .

“Sitaki kuzungumzia jambo hilo.”

Wazazi wako wanaelewa . . .

“Nitazungumza kwa uhuru na rafiki zangu, lakini ninyi si watu wa maana sana maishani mwangu ili nizungumze nanyi.”

Unaposema . . .

“Hamwezi kuelewa.”

Wazazi wako wanaelewa . . .

“Ninyi ni wazee sana na mmepitwa na wakati. Hamwezi kuelewa ulimwengu wa sasa.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Niliwaambia wazazi wangu kuhusu tatizo nililokuwa nalo shuleni na nilishangazwa na jinsi walivyonisikiliza kwa utayari. Ilikuwa rahisi kutatua tatizo hilo kwa msaada wao!”—Natalie.

“Si rahisi nyakati zote kuzungumza na wazazi wako, lakini unapozungumza nao, unahisi ni kana kwamba mzigo mzito umeondolewa katika akili yako.”—Devenye.

[Sanduku katika ukurasa wa 21]

TAARIFA KWA WAZAZI

Ukiwa mzazi mwenye kujali, huenda ukajiuliza ikiwa ni vigumu kwa watoto wako kuzungumza nawe. Ona mambo ambayo vijana fulani walimwambia mwandishi wa Amkeni! kuhusu sababu zinazowazuia wasizungumze na wazazi wao. Kisha, jiulize maswali yaliyo hapo, na usome maandiko yaliyotajwa.

Ni vigumu kwangu kuzungumza na Baba kwa sababu ana mambo mengi sana ya kufanya, kazini na kutanikoni. Ni kana kwamba hana wakati wa kuzungumza nami.—Andrew.

‘Je, nimefanya ionekane kana kwamba nina shughuli nyingi sana hivi kwamba sina wakati wa kuzungumza na vijana wangu? Ikiwa ndivyo, ninaweza kufanya nini ili waweze kunifikia kwa uhuru? Ninaweza kutenga wakati gani hususa wa kuzungumza na watoto wangu?’—Kumbukumbu la Torati 6:7.

Nilimwendea mama yangu nikilia na kumweleza kuhusu mabishano niliyokuwa nayo shuleni. Nilitaka anifariji lakini alinikemea tu. Tangu wakati huo, sijazungumza naye kuhusu jambo lolote muhimu.—Kenji.

‘Mimi hufanya nini watoto wangu wanaponijia wakiwa na tatizo? Hata ikiwa wanahitaji kusahihishwa, je, ninaweza kujifunza kunyamaza, kusikiliza, na kuelewa hisia zao kabla ya kutoa mashauri?’—Yakobo 1:19.

Ni kana kwamba kila wakati wazazi wanaposema tunaweza kuwaambia chochote na hawatakasirika, wao hukasirika. Kisha kijana anahisi kwamba amesalitiwa.—Rachel.

‘Mtoto wangu anaponiambia jambo lenye kukasirisha, ninaweza kujizuiaje nisikasirike?’—Methali 10:19.

Mara nyingi nilipozungumza na Mama kuhusu mambo ya siri, alienda na kuwaambia rafiki zake. Niliacha kumwamini kwa muda mrefu sana.—Chantelle.

‘Je, mimi humwonyesha mtoto wangu kwamba ninajali hisia zake kwa kutoeneza mambo ya siri ambayo ameniambia?’—Methali 25:9.

Kuna mambo mengi sana ninayotaka kuwaambia wazazi wangu. Ninahitaji tu msaada wa kuanzisha mazungumzo.—Courtney.

‘Je, ninaweza kuchukua hatua ya kwanza kuzungumza na kijana wangu? Ni wakati gani mzuri wa kuzungumza naye?’Mhubiri 3:7.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Hakuna kitu kinachopaswa kuzuia kabisa mazungumzo; unaweza kutafuta njia ya kuzungumza na wazazi wako!