Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Sawa Kuiba Mtihani?

Je, Ni Sawa Kuiba Mtihani?

Je, Ni Sawa Kuiba Mtihani?

JE, WEWE ni mwanafunzi? Ikiwa ndivyo, basi unawafahamu wanafunzi wenzako ambao huiba mtihani darasani ili wapate alama za juu. Kwa kweli, tatizo hilo limeenea sana. Mnamo 2008, Taasisi ya Josephson iliwahoji wanafunzi 30,000 hivi wa shule za sekondari nchini Marekani, na asilimia 64 walikubali kwamba katika mwaka huo waliiba mtihani. Hata hivyo, wengine wanakadiria kwamba huenda idadi ya wanaoiba ikawa ya juu zaidi​—zaidi ya asilimia 75.

Barani Ulaya, tatizo hilo limeenea pia, hasa tatizo la watu kuchukua mitihani ya wengine na kudai kuwa ni yao. “Tovuti zinazouza insha za wanafunzi, tasnifu za shahada ya pili na za shahada ya tatu ni tatizo jipya na linalozidi kuongezeka,” inasema makala iliyochapishwa katika jarida la Intaneti Digithum.

Kwa nini kuiba mtihani kumekuwa tatizo kubwa hivyo? Je, kweli wale wanaoiba mtihani wanafaidika? Je, kuna faida za kuwa mnyoofu​—hata ikiwa utapata alama za chini?

Kwa Nini Kuiba Mtihani Kumeenea?

Kuzorota kwa maadili. “Walimu wengi wanasema kwamba visa vya watu kuiba mitihani vimeongezeka kwa sababu watu wanajifikiria wenyewe tu na hivyo hakuna mtu aliye na maadili ya juu,” linasema jarida American School Board Journal. Mwanafunzi mmoja alisema hivi kuhusu madarasa aliyosomea katika shule ya sekondari yaliyokusudiwa kuwatayarisha wanafunzi kwa ajili ya chuo kikuu: “Sisi sote . . . tuliiba; tulihitaji kupata alama za juu ili tukubaliwe katika shule nzuri. Sote tulikuwa wanafunzi wazuri walio na maadili mazuri; hatukuwa watu wasiofuata kanuni . . . Ni kwamba tu tulihitaji kuingia katika vyuo vikuu vizuri.” Hata wazazi fulani wameanza kuwa na maoni hayo. Kwa kuwa wanataka sana watoto wao “wafaulu,” wao hupuuza au kukubali watoto waibe mitihani, na hivyo kuathiri maadili ya watoto hata zaidi.

Shinikizo la kufanikiwa. Kulingana na Donald McCabe, mwanzilishi wa Kituo cha Kimataifa cha Kuweka Viwango vya Maadili Katika Elimu, wanafunzi ambao huiba mitihani wanaamini kwamba kuendelea kuwa wanyoofu ni hasara kwao iwapo watafanya mtihani uleule na wengine wanaoiba mtihani bila kushikwa.

Msaada wa teknolojia. Teknolojia ya kisasa inawawezesha wanafunzi kuiba kwa njia rahisi na za hali ya juu zaidi. Wanaweza kupakua kutoka kwenye Intaneti karatasi za mitihani pamoja na majibu ya kazi walizopewa wafanyie nyumbani na kuwasambazia wengine. Mara nyingi ni watu wachache tu wanaoshikwa, na kwa sababu hiyo wengine hupata ujasiri wa kuiba.

Uvutano wa mifano mibaya. Kuiba kumekuwa jambo la kawaida hata kati ya watu wazima​—katika makampuni makubwa, katika siasa, katika michezo, na mara nyingi hata nyumbani, ambako wazazi hudanganya kuhusu kodi au bima. “Ikiwa watu walio na mamlaka au wale wanaopaswa kuigwa wanasema uwongo,” anasema David Callahan, mwandishi wa kitabu The Cheating Culture, “basi nafikiri vijana wanapata wazo la kwamba kusema uwongo ni sawa tu.” Lakini je, ni sawa kusema uwongo? Je, kutaka kupata alama za juu kunafanya iwe sawa kuiba mtihani?

Kwa Nini Mtu Aepuke Kuiba Mtihani?

Jiulize hivi, ‘Ni nini kusudi la kupata elimu nzuri? ’ Je, si kuwatayarisha wanafunzi kwa ajili ya madaraka mengi watakayokuwa nayo maishani, kama vile kuchanganua matatizo kazini na kuyatatua? Wanafunzi wanaokuwa na zoea la kuiba mtihani huenda wakakosa kujifunza ustadi huo muhimu. Kwa hiyo, watu ambao wana zoea la kudanganya wanaficha udhaifu wao na wanapunguza uwezekano wao wa kufaulu katika sehemu nyingi maishani.

Zaidi ya hilo, “watu ambao huchagua kufuata njia za mkato maishani​—kama vile kuwa na zoea la kuiba mitihani shuleni​—wanaweza kuendeleza zoea hilo wanapoajiriwa,” anasema Callahan. Kwa njia fulani, watu hao ni kama vazi au saa inayoonekana kuwa ya hali ya juu lakini ni bandia na mwishowe inakatisha tamaa.

Bila shaka, watu wanaoiba mitihani wanakabili hatari ya kushikwa na kuadhibiwa. Huenda wakaaibishwa. Huenda pia wakafukuzwa shuleni au wakapewa adhabu kali zaidi. Biblia inaonya hivi waziwazi: “Lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.” (Wagalatia 6:7) Hata hivyo, mtu hapaswi kuwa mnyoofu kwa sababu tu ya kuogopa kushikwa. Kuna sababu zinazofaa zaidi.

Unyoofu​—Ufunguo Halisi wa Kupata Mafanikio

Vijana wenye hekima hujitahidi kusitawisha sifa ambazo zitawafaidi, si shuleni tu, bali katika maisha yao yote. Hivyo, wao hutia bidii shuleni na kujitahidi kusitawisha sifa ambazo huwasaidia wajiheshimu, sifa ambazo zitawafanya wapendwe na waajiri wao wakati ujao, na zitakazowaletea furaha ya kudumu.

Sifa hizo zinaweza kupatikana katika Biblia, na vijana wanaoishi kupatana nazo hawapati hasara. Badala yake, kama 2 Timotheo 3:​16, 17 inavyosema, wanakuwa ‘na uwezo kamili, wakiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’ Mwanafunzi anayeitwa Jorge anasema hivi: “Wanafunzi wenzangu huiba mitihani kwa sababu wanataka kupata alama za juu bila kutia jitihada nyingi. Lakini mimi ninataka kumpendeza Mungu. Katika Methali 14:​2, Biblia inasema kwamba ‘anayetembea katika unyoofu wake anamwogopa Yehova, lakini mtu mpotovu anamdharau Yeye katika njia zake.’ Ninajua kwamba hatuwezi kumficha Mungu chochote. Kwa hiyo, mimi huwa siibi, wala siwasaidii wengine kufanya hivyo.”

Wanafunzi wanaojitahidi kuishi kupatana na kanuni za Biblia wanaweza kuwa au huenda wasiwe wanafunzi werevu zaidi darasani. Lakini wao ni wenye hekima zaidi, kwa kuwa wanaweka msingi imara wa kuwa na maisha yenye mafanikio ya kudumu. (Zaburi 1:​1-3; Mathayo 7:​24, 25) Isitoshe, wanahakikishiwa kwamba watapata kibali na utegemezo wa Muumba.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 28]

KANUNI UNAZOPASWA KUFIKIRIA

● “Mdomo wa ukweli ndio utakaofanywa imara milele, lakini ulimi wa uwongo ni wa muda mfupi tu.”​—Methali 12:19.

● “Mtu mwenye matendo ya uaminifu atapata baraka nyingi.”​—Methali 28:20.

● “Mungu wa kweli ataleta kila kazi katika hukumu, kuhusiana na kila jambo lililofichwa, liwe jema au baya.”​—Mhubiri 12:14.

● “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”​—Waebrania 13:18.

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Teknolojia ya kisasa inawawezesha wanafunzi kuiba mtihani kwa njia rahisi na za hali ya juu

[Picha katika ukurasa wa 28]

Wanafunzi ambao huiba mitihani ni kama saa inayoonekana kuwa ya hali ya juu lakini ni bandia ambayo kwa nje inaonekana kuwa nzuri