Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwisho wa Dunia Huenda Usije kwa Njia Unayofikiri

Mwisho wa Dunia Huenda Usije kwa Njia Unayofikiri

MBALI na kuashiria mabaya, mambo yaliyotajwa katika makala zilizotangulia kuhusu mwisho wa dunia yanafanana katika njia tatu. Kwanza yanategemea makisio ya wanadamu, na historia inaonyesha kwamba wanadamu hawawezi kutabiri wakati ujao. Pili, ikiwa kuna wanadamu wowote watakaookoka, itakuwa kwa sadfa tu. Tatu, waokokaji wa mwisho wa dunia wataishi maisha magumu sana.

Tofauti na hilo, yale ambayo Biblia inasema kuhusu wakati ujao yanapatana zaidi na akili. Biblia inasema kwamba kwa kweli kuna mabadiliko makubwa yanayokuja. Lakini wale wanaofanya mapenzi ya Mungu wataokoka hakika. Isitoshe, Biblia haisemi kwamba dunia italipuliwa iwe majivu au itageuka kuwa barafu. Badala yake, dunia nzima itageuzwa kuwa paradiso.

Hata hivyo, watu wengi wanaona vigumu sana kuamini matabiri hayo ya Biblia. Watu walio na shaka huona kuwa yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu dhiki kuu, Har–Magedoni, kipindi cha miaka elfu, na Paradiso ni mambo ya kuwaziwa tu. Kwa muda mrefu mafundisho hayo yamejadiliwa, kubishaniwa, na kufasiriwa na wanatheolojia. Maoni yao yanapingana. Mwandishi Bruce A. Robinson anasema hivi kuhusu wakati wa mwisho: “Kati ya mafundisho yote ya dini zinazodai kuwa za Kikristo, huenda hakuna maandishi mengine ya kitheolojia ambayo yameandikwa kwa njia isiyoeleweka wazi kuliko hayo.” Matokeo yamekuwa nini? Vurugu.

Ingawa hivyo, Maandiko hayaelezi mambo katika njia isiyoeleweka. Biblia ni ujumbe kutoka kwa Mungu, naye hataki tutatanishwe kuhusu yatakayotukia wakati ujao. Chunguza baadhi ya maswali ambayo huulizwa mara nyingi, na yale ambayo Biblia yenyewe inasema. Ikiwa ungependa kujifunza mengi zaidi, unaweza kuomba kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, dunia pamoja na wanadamu wote wataharibiwa?

“Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”​—Zaburi 37:29.

Je, kuna wanadamu wowote ambao watakufa?

“Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.”​—Methali 2:21, 22.

Je, Mungu amewahi kuwaharibu watu wasiomwogopa nyakati za kale?

Mungu “hakujizuia kuuadhibu ulimwengu wa kale, bali alimlinda Noa, mhubiri wa uadilifu, akiwa salama pamoja na wengine saba alipoleta gharika juu ya ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu; na kwa kuyageuza majiji ya Sodoma na Gomora kuwa majivu aliyahukumia adhabu, akiweka kielelezo kwa watu wasiomwogopa Mungu juu ya mambo yatakayokuja.”—2 Petro 2:5, 6.

Tunaweza kujua tarehe ambayo Mungu ataleta hukumu?

“Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu. Kwa maana kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa. Kwa maana kama vile walivyokuwa katika siku hizo kabla ya gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.”​—Mathayo 24:36-39.

Je, kuna dalili zozote zinazoonyesha kwamba mwisho utakuja hivi karibuni?

“Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake.”​—2 Timotheo 3:1-5.

Wanadamu walio duniani watarajie nini wakati ujao?

Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.

Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao”

Ingawa Maandiko hayatuelezi kila kitu kuhusu wakati ujao, yanatuhakikishia kwamba kuna tumaini. Wakati ujao utakuwa mtukufu kuliko tunavyoweza kuwazia. Unaweza kuamini jambo hilo ukiwa na uhakika kwamba Yehova Mungu anaweza kutimiza kile ambacho ameahidi.