Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni Ya Biblia

Je, Mungu Anatumia Misiba ya Asili Kuwaadhibu Wanadamu Leo?

Je, Mungu Anatumia Misiba ya Asili Kuwaadhibu Wanadamu Leo?

WATU fulani wanaamini kwamba Mungu anatumia misiba ya asili kuwaadhibu wanadamu. Wengine wanapinga wazo hilo. Na wengine hawajui waamini nini. Profesa mmoja wa mambo ya dini alisema hivi: “Mafundisho mengi ya dini yanaonyesha kwamba hakuna mtu anayeweza kusema kwa uhakika kwamba misiba ya asili ni mapenzi ya Mungu.”

Hata hivyo, Biblia ina majibu yenye kuridhisha. Inatusaidia kuelewa kama kweli Mungu hutumia misiba ya asili kuwaadhibu wanadamu leo. Pia inatueleza ni kwa nini watu wengi wanateseka.

Maandiko Yanatoa Kielelezo

Biblia inafunua kweli mbili za msingi kuhusu Mungu ambaye jina lake ni Yehova. Kwanza, yeye ndiye Muumba na kwa hiyo ana nguvu na mamlaka ya kudhibiti nguvu za asili za dunia. (Ufunuo 4:11) Pili, sikuzote matendo yake hupatana na utu, sifa, na kanuni zake. Anasema hivi kwenye Malaki 3:6: “Mimi ni Yehova; sikubadilika.” Ukiwa na mambo hayo akilini, chunguza matukio mawili ya kale, moja kuhusu gharika na lingine kuhusu ukame. Utaona kwamba katika historia ya Biblia, wakati Mungu alipotumia nguvu za asili kutekeleza hukumu zake, sikuzote alitoa (1) onyo, (2) sababu, na (3) ulinzi kwa ajili ya waabudu wake watiifu.

Gharika ya Siku za Noa

Onyo.

Miaka mingi kabla ya Gharika, Yehova alimwambia Noa: “Mimi ninaleta gharika ya maji duniani ili kuharibu kutoka chini ya mbingu wote wenye mwili.” (Mwanzo 6:17) Noa “mhubiri wa uadilifu,” aliwaonya watu, lakini “hawakujali.”​—2 Petro 2:5; Mathayo 24:39.

Sababu.

Yehova alitangaza hivi: “Mwisho wa wote wenye mwili umekuja mbele zangu, kwa maana dunia imejaa jeuri kwa sababu yao.”​—Mwanzo 6:13.

Ulinzi kwa ajili ya waabudu wake watiifu.

Yehova alimpa Noa maagizo hususa kuhusu ujenzi wa safina ambayo ingewaokoa watu wakati wa Gharika. “Noa peke yake na wale waliokuwa pamoja naye ndani ya safina wakaendelea kuwa hai.”​—Mwanzo 7:23.

Ukame Israeli

Onyo.

Kabla ya Yehova Mungu kuleta ukame mbaya sana huko Israeli, nabii wake Eliya alitangaza hivi: “Miaka hii hakutakuwa na umande wala mvua, isipokuwa kwa agizo la neno [la Mungu]!”​—1 Wafalme 17:1.

Sababu.

Mungu alileta ukame huo kwa sababu Waisraeli walimwabudu Baali, mungu wa uwongo. Eliya alieleza hivi: ‘Ninyi mmeziacha amri za Yehova, nanyi mkaanza kufuata Mabaali.’​—1 Wafalme 18:18.

Ulinzi kwa ajili ya waabudu wake watiifu.

Yehova aliwaandalia waabudu wake watiifu chakula wakati wa ukame huo.​—1 Wafalme 17:6, 14; 18:4; 19:18.

Vielelezo Hivyo Vinafunua Nini?

Leo hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba misiba ya asili ni njia ya kuwaadhibu wanadamu. Kwa kuwa yeye ni Mungu wa haki, Yehova hajawahi ‘kumfagilia mbali mwadilifu pamoja na mwovu.’ (Mwanzo 18:23, 25) Aliwalinda wale waliomtii. Leo misiba ya asili huwakumba wanaume, wanawake, na watoto bila kubagua.

Mungu hawezi kuwa ndiye anayesababisha misiba inayowadhuru watu

Ni wazi kwamba misiba ya asili inayotukia leo haifuati kielelezo cha misiba iliyoletwa na Mungu inayopatikana katika Maandiko. Isitoshe, matukio hayo ya hapa na pale hayapatani na utu wa Mungu. Andiko la Yakobo 1:13 linasema kwamba Mungu hawajaribu watu na mambo maovu, na 1 Yohana 4:8 inaelezea utu wa Mungu kwa kusema “Mungu ni upendo.” Yeye hawezi kuwa ndiye anayesababisha dhoruba, matetemeko ya nchi, na misiba mingine ambayo huwadhuru watu wasio na hatia. Je, misiba kama hiyo itawahi kwisha?

Kuteseka Kutakwisha

Yehova Mungu hakukusudia wanadamu wakumbwe na misiba ya asili. Mapenzi yake ni kwamba wanadamu waishi milele chini ya hali zenye amani duniani. Kama alivyofanya katika siku za Noa, ataingilia shughuli za wanadamu na kuondoa uovu. Sawa na alivyofanya hapo zamani, Yehova Mungu anatoa onyo mapema kupitia ujumbe unaotangazwa ulimwenguni pote, hivyo anawapa watu fursa ya kujitayarisha kwa ajili ya wokovu.​—Zaburi 37:9, 11, 29; Mathayo 24:14.