Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kubaki Imara Mtoto Anapoasi

Kubaki Imara Mtoto Anapoasi

Kubaki Imara Mtoto Anapoasi

MWANAMKE mmoja Mkristo ambaye tutamwita Joy alijitahidi kumlea mwana wake ili ampende Yehova Mungu. Hata hivyo, alipokuwa tineja, mwana huyo aliasi na kuondoka nyumbani. Joy anasema hivi: “Hilo ni jambo ambalo liliniumiza zaidi. Nilihisi nimesalitiwa, nimevunjika moyo, na kufadhaika. Nililemewa sana na maoni yasiyofaa.”

Pengine wewe pia umejitahidi kuwalea watoto wako ili wampende na kumtumikia Mungu, lakini mmoja wao au watoto kadhaa wanamwasi. Unaweza kukabiliana kwa njia gani na uchungu huo wenye kuvunja moyo? Ni nini kitakachokusaidia kubaki imara katika utumishi wako kwa Yehova?

Wakati Wana wa Yehova Walipoasi

Hatua ya kwanza ni kutambua kwamba Yehova anaelewa kabisa jinsi unavyohisi. Tunasoma hivi katika Isaya 49:15: “Je, mke anaweza kumsahau mtoto wake anayenyonya hivi kwamba asimhurumie mwana wa tumbo lake? Hata hawa wanawake wanaweza kusahau, lakini mimi mwenyewe sitakusahau wewe.” Ndiyo, Yehova ana hisia ambazo kwa kawaida baba na mama wanakuwa nazo. Basi, wazia jinsi alivyofurahi wanawe wote wa kimalaika walipokuwa wakimsifu na kumtumikia. Akimjibu mzee wa ukoo Ayubu kutoka katika “dhoruba ya upepo,” Yehova alikumbuka pindi zenye furaha alipokuwa na familia yake yenye umoja ya viumbe wa roho. Alisema hivi: “Ulikuwa wapi nilipoweka msingi wa dunia? . . . Nyota za asubuhi zilipopiga vigelegele pamoja kwa shangwe, na wana wote wa Mungu wakaanza kupaaza sauti kwa kushangilia?”—Ayubu 38:1, 4, 7.

Baada ya muda, Mungu wa kweli aliona mwana mkamilifu wa kimalaika akimwasi na kuwa Shetani, jina linalomaanisha “Mpinzani.” Pia, Yehova alimwona mwana wake wa kwanza wa kibinadamu, Adamu, na mke wake mkamilifu, Hawa, wakiunga mkono uasi huo. (Mwanzo 3:1-6; Ufunuo 12:9) Baadaye, wana wengine wa kimalaika ‘waliyaacha makao yao wenyewe yanayofaa’ na kumwasi Mungu.—Yuda 6.

Maandiko hayatuambii jinsi Yehova alivyohisi wakati wanawe fulani wakamilifu walipoasi. Hata hivyo, Biblia inasema hivi waziwazi: “Yehova akaona kuwa ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani na kila mwelekeo wa fikira za moyo wake ulikuwa mbaya tu wakati wote. Yehova akajuta kwamba amewafanya wanadamu duniani, naye akaumia moyoni mwake.” (Mwanzo 6:5, 6) Pia, uasi wa Israeli, watu wa Yehova waliochaguliwa, ‘ulimhuzunisha’ na ‘kumtia uchungu.’—Zaburi 78:40, 41.

Hapana shaka kwamba Yehova anawahurumia wazazi ambao wanahisi uchungu na kuumia moyoni kwa sababu ya mwenendo wa watoto wao wanaoasi. Katika Neno lake, Biblia, ametoa mashauri mazuri na kitia-moyo ili kuwasaidia wazazi kama hao wakabiliane na hali yao. Mungu anawahimiza wamtupie mahangaiko yao, wajinyenyekeze, na wachukue msimamo na kumpinga Shetani Ibilisi. Acha tuone jinsi kufuata mashauri hayo kunavyoweza kukusaidia ubaki imara mtoto wako anapoasi.

Mtupie Yehova Mahangaiko Yako

Yehova anajua kwamba kati ya mambo machache ambayo yanawahangaisha sana wazazi ni kutambua kwamba watoto wao wanaweza kujiumiza wenyewe au kuumizwa na wengine. Mtume Petro anaonyesha njia moja ya kukabiliana na hangaiko hilo na mahangaiko mengine. Anaandika: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu ya Yehova, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’ (1 Petro 5:7) Kwa nini mwaliko na uhakikisho huo unaweza kuwasaidia sana wazazi ambao mtoto wao ameasi?

Mtoto wako alipokuwa mchanga, ulimlinda kwa bidii kutokana na hatari, na inaelekea kwamba alifuata mwongozo wako wenye upendo. Hata hivyo, alipoendelea kukua, huenda uvutano wako juu yake ulipungua, lakini bidii yako ya kumlinda haikupungua. Inaelekea kwamba bidii hiyo iliongezeka.

Kwa hiyo, mtoto wako anapoasi na kuumia kiroho, kihisia, au kimwili, huenda ukajilaumu. Joy, aliyetajwa mwanzoni, alihisi hivyo. Anasema hivi: “Kila siku, nilisumbuka nikihisi kwamba sikufaulu, niliendelea kufikiria matukio yaliyopita.” Wakati kama huo hasa, ndipo Yehova anapotaka ‘utupe mahangaiko yako yote juu yake.’ Ukifanya hivyo atakusaidia. Mtunga-zaburi alisema: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.” (Zaburi 55:22) Joy alipata faraja kama hiyo. Anaeleza hivi: “Nilimweleza Yehova kwa undani kuhusu hisia zangu zote za moyoni. Nilimmwagia hisia zangu, nami nikahisi nimetulia sana.”

Ukiwa mzazi ambaye si mkamilifu, huenda ulifanya makosa fulani katika kumlea mtoto wako. Lakini mbona ukazie fikira makosa yako tu? Bila shaka, Yehova hafanyi hivyo, kwa kuwa mtunga-zaburi aliimba hivi: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Huenda mtoto wako angeasi hata kama hungekosea. Hivyo, mweleze Yehova katika sala jinsi unavyohisi, naye atakusaidia kukabiliana na hali hiyo. Hata hivyo, unapaswa kufanya mengi zaidi ili ubaki imara katika kumtumikia Yehova na kuepuka kunaswa na Shetani.

Jinyenyekeze

Petro aliandika hivi: “Jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue ninyi katika wakati unaofaa.” (1 Petro 5:6) Kwa nini unyenyekevu unahitajiwa mtoto wako anapoasi? Zaidi ya kukutia uchungu na kukufanya uhisi una hatia, kuwa na mtoto mwasi kunaweza kukuaibisha. Huenda ukahangaika kwamba matendo ya mtoto wako yameharibu sifa njema ya familia yako, hasa ikiwa ametengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo. Kuwa na hisia za kujilaumu na kuaibishwa kunaweza kukuvunja moyo usihudhurie mikutano ya Kikristo.

Unaposhughulika na hali kama hiyo unahitaji kuwa na hekima inayotumika. Andiko la Methali 18:1 linaonya hivi: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” Ingawa una huzuni, ukihudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida utapata maagizo na kitia-moyo. “Mwanzoni, sikutaka kukutana na yeyote,” anasema Joy. “Lakini nilijikumbusha umuhimu wa mazoea yangu mazuri ya kiroho. Pia, ikiwa ningekaa nyumbani, ningefikiria tu matatizo yangu. Mikutano ilinisaidia kukazia fikira mambo ya kiroho yenye kujenga. Ninafurahi sana kwamba sikujitenga na wengine na kukosa kufaidika kutokana na utegemezo wenye upendo wa ndugu na dada zangu.”—Waebrania 10:24, 25.

Pia, kumbuka kwamba ni lazima kila mmoja katika familia ‘abebe mzigo wake mwenyewe’ wa wajibu wa Kikristo. (Wagalatia 6:5) Yehova anawatazamia wazazi wawapende na kuwatia nidhamu watoto wao. Pia, anawatazamia watoto wawatii na kuwaheshimu wazazi wao. Wazazi wakijitahidi wawezavyo kuwalea watoto wao katika “nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova,” wazazi wenyewe watakuwa na sifa njema machoni pa Mungu. (Waefeso 6:1-4) Mtoto akiasi nidhamu yenye upendo ya wazazi, sifa yake ndiyo itakayoharibika. Andiko la Methali 20:11 linasema hivi: “Kwa matendo yake, mvulana hujitambulisha kama utendaji wake ni safi na mnyoofu.” Uasi wa Shetani haujaharibu sifa njema ya Yehova machoni pa wale wanaojua ukweli wa mambo.

Chukua Msimamo Ukampinge Ibilisi

Petro anaonya hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Petro 5:8) Kama simba, sikuzote Ibilisi analenga vijana na wale wasio na uzoefu. Katika nyakati za kale, simba walizunguka-zunguka huko Israeli na walikuwa hatari kwa wanyama wa kufugwa. Ikiwa mwana-kondoo angejitenga na kundi, angeshambuliwa kwa urahisi. Kwa kawaida, kondoo-jike angehatarisha uhai wake ili kumlinda mwana-kondoo wake. Lakini, hata kondoo mkubwa hangeweza kumshinda simba. Hivyo, wachungaji wajasiri walihitajiwa ili kulilinda kundi.—1 Samweli 17:34, 35.

Ili kuwalinda kondoo wake wa mfano wasimezwe na “simba anayenguruma,” Yehova ameandaa wachungaji wa kiroho walichunge kundi chini ya “mchungaji mkuu,” Yesu Kristo. (1 Petro 5:4) Petro anawapa wanaume waliowekwa rasmi himizo hili: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu.” (1 Petro 5:1, 2) Ninyi wazazi mkishirikiana na wachungaji, wachungaji hao wanaweza kumsaidia kijana wenu arekebishe hali yake ya kiroho.

Wachungaji Wakristo wanapohitaji kumshauri mtoto wako aliyeasi, huenda ukataka kumlinda asitiwe nidhamu. Lakini, hilo lingekuwa kosa kubwa. Petro anasema hivi: “Chukueni msimamo mkampinge [Ibilisi],” wala hasemi mkawapinge wachungaji wa kiroho.—1 Petro 5:9.

Nidhamu Kali Inapotolewa

Mtoto wako asipotubu na ikiwa yeye ni Mkristo ambaye amebatizwa, huenda akatiwa nidhamu kali, yaani, kutengwa na ushirika wa kutaniko. Kuanzia hapo na kuendelea, uhusiano wako na yeye utategemea umri wake na hali nyingine.

Ikiwa mtoto huyo hajafikia umri wa kutambuliwa kisheria kuwa mtu mzima na anaishi nyumbani, utahitaji kuendelea kumtimizia mahitaji yake ya kimwili. Pia, anahitaji mafundisho na nidhamu, nawe una wajibu wa kutimiza uhitaji huo. (Methali 1:8-18; 6:20-22; 29:17) Huenda ukataka kujifunza naye Biblia, na kumhusisha moja kwa moja. Unaweza kumwonyesha maandiko mbalimbali na vichapo ambavyo vimechapishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Unaweza pia kwenda naye kwenye mikutano ya Kikristo na kuketi pamoja naye. Unaweza kufanya yote hayo ukitumaini kwamba atatii mashauri ya Kimaandiko.

Hali ni tofauti ikiwa aliyetengwa na ushirika anatambuliwa kisheria kuwa mtu mzima na haishi nyumbani. Mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo katika Korintho la kale: “Mwache kuchangamana katika ushirika pamoja na mtu yeyote anayeitwa ndugu ambaye ni mwasherati au mtu mwenye pupa au mwabudu-sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi, hata msile chakula pamoja na mtu wa namna hiyo.” (1 Wakorintho 5:11) Mnaposhughulikia mambo ya lazima ya familia huenda mkahitaji kushirikiana na mtu aliyetengwa na ushirika, hata hivyo mzazi Mkristo atajitahidi kuepuka kushirikiana isivyo lazima na mtu huyo.

Mtoto aliyekosea anapotiwa nidhamu na wachungaji Wakristo, halingekuwa jambo la hekima kwa mzazi kukataa au kupunguza uzito wa nidhamu ambayo inategemea Biblia. Kumtetea mtoto wako aliyeasi hakuwezi kumlinda kutokana na Ibilisi. Kwa kweli, utakuwa ukihatarisha hali yako mwenyewe ya kiroho. Kwa upande mwingine, unapounga mkono jitihada za wachungaji, utabaki “imara katika imani” nawe utakuwa umemsaidia kabisa mtoto wako.—1 Petro 5:9.

Yehova Atakutegemeza

Mtoto wako akiasi, kumbuka kwamba huko peke yako. Wazazi wengine Wakristo wamekabili hali kama yako. Hata tukikabili majaribu ya aina gani, Yehova anaweza kututegemeza.—Zaburi 68:19.

Mtegemee Yehova katika sala. Shirikiana kwa ukawaida na kutaniko la Kikristo. Unga mkono nidhamu inayotolewa na wachungaji waliowekwa rasmi. Kwa kufanya hivyo, utafaulu kubaki imara. Na mfano wako mzuri unaweza kumsaidia mtoto wako akubali mwaliko wenye upendo kutoka kwa Yehova wa kumrudia.—Malaki 3:6, 7.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Jitie nguvu kwa kusali na kwa kushirikiana na kutaniko la Kikristo