Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unafuata “Njia Iliyo Bora Zaidi” Ya Upendo?

Je, Unafuata “Njia Iliyo Bora Zaidi” Ya Upendo?

Je, Unafuata “Njia Iliyo Bora Zaidi” Ya Upendo?

“MUNGU ni upendo.” Maneno hayo ya mtume Yohana yanafunua sifa kuu zaidi ya Mungu. (1 Yoh. 4:8) Upendo wa Mungu kwa wanadamu ndio unaotuwezesha kumkaribia na kuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja naye. Upendo wa Mungu una uvutano gani mwingine juu yetu? Inasemekana kwamba “mambo tunayopenda yana uvutano juu ya maisha yetu.” Na hilo ni kweli. Hata hivyo, ni kweli pia kwamba watu tunaowapenda na wale wanaotupenda wana uvutano juu ya maisha yetu. Kwa kuwa tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, tunaweza kuonyesha upendo wa Mungu katika maisha yetu. (Mwa. 1:27) Kwa hiyo, mtume Yohana aliandika kwamba tunampenda Mungu “kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.”—1 Yoh. 4:19.

Maneno Manne Yanayofafanua Upendo

Mtume Paulo alisema kwamba upendo ndiyo “njia iliyo bora zaidi.” (1 Kor. 12:31) Kwa nini alitumia maneno hayo kuufafanua upendo? Paulo alikuwa akizungumza kuhusu upendo wa aina gani? Ili kupata jibu, acheni tuchunguze kwa undani maana ya neno “upendo.”

Wagiriki wa zamani walikuwa na maneno manne ya msingi, yaliyotumiwa kwa njia mbalimbali kueleza kuhusu upendo: stor·geʹ, eʹros, phi·liʹa, na a·gaʹpe. Kati ya maneno hayo, neno a·gaʹpe ndilo neno linalotumiwa kueleza kuhusu Mungu ambaye “ni upendo.” * Kuhusu upendo huo, Profesa William Barclay anasema hivi katika kitabu chake (New Testament Words): “Upendo wa Agapē unahusiana na akili: si hisia tu inayojitokeza yenyewe katika mioyo yetu; ni kanuni ambayo tunachagua kuishi kupatana nayo bila kulazimishwa. Upendo wa Agapē unategemea hasa hiari” au kupenda. Katika hali hii, a·gaʹpe ni upendo unaoongozwa na kanuni, lakini mara nyingi unaambatana na hisia zenye nguvu. Kwa kuwa kuna kanuni nzuri na mbaya, ni wazi kwamba Wakristo wanapaswa kuongozwa na kanuni nzuri ambazo Yehova Mungu mwenyewe ameweka katika Biblia. Tunapolinganisha maelezo ya Biblia kuhusu a·gaʹpe na maneno mengine yanayotumiwa katika Biblia kuelezea upendo, tutaelewa vizuri zaidi upendo ambao tunapaswa kuonyesha.

Upendo Katika Familia

Inapendeza kama nini kuwa katika familia yenye upendo na umoja! Neno la Kigiriki stor·geʹ lilitumiwa mara nyingi kurejelea upendo wa asili kati ya washiriki wa familia ileile. Wakristo wanajitahidi kuwapenda washiriki wa familia yao. Paulo alitabiri kwamba katika siku za mwisho, kwa ujumla watu ‘hawangekuwa na upendo wa asili.’ *2 Tim. 3:1, 3.

Inahuzunisha kwamba upendo wa asili ambao unapaswa kuwapo kati ya washiriki wa familia unakosekana katika ulimwengu wa leo. Kwa nini wanawake wengi wajawazito wanatoa mimba? Kwa nini familia nyingi sana zinawapuuza wazazi wao waliozeeka? Kwa nini talaka zinazidi kuongezeka? Kwa kweli jibu ni kwamba watu hao hawana upendo wa asili.

Kwa kuongezea, Biblia inafundisha kwamba “moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote.” (Yer. 17:9) Upendo wa familia unahusiana na moyo wetu na hisia zetu. Hata hivyo, inapendeza kujua kwamba Paulo alitumia neno a·gaʹpe kueleza kuhusu upendo ambao mume anapaswa kumwonyesha mke wake. Paulo alilinganisha upendo huo na upendo ambao Kristo analionyesha kutaniko. (Efe. 5:28, 29) Upendo huo unategemea kanuni zilizowekwa na Yehova, Mwanzilishi wa mpango wa familia.

Upendo wa kweli kwa washiriki wa familia unatuchochea kupendezwa na wazazi wetu waliozeeka au unatuchochea kutimiza daraka la kuwatunza watoto wetu. Unawachochea pia wazazi kuwatia nidhamu watoto wao kwa upendo inapohitajika na unawazuia wazazi kutenda tu kwa hisia, jambo ambalo mara nyingi linawafanya wazazi wawaache watoto wafanye jambo lolote wanalotaka.—Efe. 6:1-4.

Upendo wa Kimahaba na Kanuni za Biblia

Kwa kweli, upendo wa kimwili kati ya mwanamume na mwanamke katika ndoa ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Met. 5:15-17) Hata hivyo, neno eʹros, ambalo linahusu upendo wa kimahaba, halitumiwi na waandikaji wa Biblia walioongozwa na roho takatifu. Kwa nini? Miaka mingi iliyopita, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilisema hivi: “Leo inaonekana kwamba ulimwengu wote unatenda kosa lilelile ambalo Wagiriki wa zamani walitenda. Walimwabudu mungu aliyeitwa Eros, waliinama katika madhabahu yake na kumtolea dhabihu. . . . Lakini historia inaonyesha kwamba ibada hiyo ya upendo wa kingono ilisababisha upotovu, uovu na maangamizo. Labda ndiyo sababu waandikaji wa Biblia hawakutumia neno hilo.” Ili tuepuke kuingia katika mahusiano kwa sababu ya kuvutiwa tu na sura ya nje, ni lazima hisia za kimahaba ziongozwe, au zidhibitiwe, na kanuni za Biblia. Basi jiulize hivi: ‘Je, hisia zangu za kimahaba zinasawazishwa na upendo wa kweli kwa mwenzi wangu?’

Wakati wa “upeo wa ujana,” wakati ambapo mara nyingi tamaa za ngono zina nguvu sana, vijana wanaoshikamana na kanuni za Biblia watabaki safi kiadili. (1 Kor. 7:36; Kol. 3:5) Tunaiona ndoa kuwa zawadi takatifu kutoka kwa Yehova. Yesu alisema hivi kuhusu wenzi wa ndoa: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mt. 19:6) Badala ya kuishi pamoja kwa sababu tu ya kuvutiana kimwili, tunachukua kwa uzito wajibu wetu wa ndoa. Ndoa inapokumbwa na matatizo, hatutafuti njia rahisi ya kutokea badala yake tunajitahidi kabisa kuonyesha sifa zinazompendeza Mungu ili maisha yetu ya familia yawe yenye furaha. Tukijitahidi kwa njia hiyo tutapata furaha ya kudumu.—Efe. 5:33; Ebr. 13:4.

Upendo Kati ya Marafiki

Maisha yangechosha sana bila marafiki! Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Yuko rafiki anayeshikamana na mtu kwa ukaribu zaidi kuliko ndugu.” (Met. 18:24) Yehova anataka tuwe na marafiki wa kweli. Watu wengi wanajua jinsi Daudi na Yonathani walivyokuwa na urafiki wa karibu sana. (1 Sam. 18:1) Na Biblia inasema kwamba Yesu ‘alimpenda’ mtume Yohana. (Yoh. 20:2) Neno la Kigiriki phi·liʹa linatafsiriwa kuwa “upendo” au “urafiki.” Si kosa kuwa na rafiki wa karibu katika kutaniko. Hata hivyo, katika 2 Petro 1:7, tunatiwa moyo tuongeze upendo (a·gaʹpe) kwenye ‘upendo wetu wa kindugu’ (phi·la·del·phiʹa, neno linalotokana na maneno mawili, phiʹlos, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “rafiki,” na a·del·phosʹ, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ndugu”). Ili kufurahia urafiki wa kudumu, tunahitaji kutumia shauri hilo. Tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, hisia zangu za urafiki zinasawazishwa na kanuni za Biblia?’

Neno la Mungu linatusaidia kuepuka kuonyesha ubaguzi tunaposhughulika na marafiki wetu. Hatupaswi kutumia viwango viwili tofauti: kiwango kisicho na masharti magumu kwa ajili ya marafiki wetu na kiwango tofauti, chenye masharti magumu kwa ajili ya watu ambao si marafiki wetu. Zaidi ya hayo, hatupaswi kuwasifu-sifu watu au kuwapaka mafuta ili wawe marafiki wetu. Jambo la maana zaidi ni kwamba tunapotumia kanuni za Biblia tunakuwa na utambuzi unaohitajiwa katika kuchagua marafiki na kuepuka ‘mashirika mabaya ambayo yanaharibu tabia nzuri.’—1 Kor. 15:33.

Kifungo cha Pekee cha Upendo!

Kwa kweli, kifungo kinachowaunganisha Wakristo ni cha pekee! Mtume Paulo aliandika hivi: “Upendo wenu na uwe bila unafiki. . . . Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake.” (Rom. 12:9, 10) Kwa kweli, Wakristo wana ‘upendo (a·gaʹpe) bila unafiki.’ Upendo huo hautegemei tu hisia inayojitokeza katika mioyo yetu. Badala yake, unategemea kabisa kanuni za Biblia. Hata hivyo, Paulo anataja pia “upendo wa kindugu” (phi·la·del·phiʹa) na “upendo mwororo” (phi·loʹstor·gos, neno linalotokana na maneno phiʹlos na stor·geʹ). Msomi mmoja anasema kwamba “upendo wa kindugu” ni “upendo unaotoka moyoni, unaoonyesha fadhili, huruma, na unaosaidia.” Upendo huo unapounganishwa na a·gaʹpe, unasitawisha uhusiano wa karibu kati ya waabudu wa Yehova. (1 The. 4:9, 10) Neno lingine ambalo limetafsiriwa kuwa “upendo mwororo,” linapatikana mara moja tu katika Biblia na linamaanisha kuwa na uhusiano wa karibu sana na mchangamfu, kama vile katika familia. *

Kifungo kinachowaunganisha Wakristo wa kweli kinatia ndani upendo wa familia na upendo kwa marafiki wa kweli, na mahusiano yote yanaongozwa na upendo unaotegemea kanuni za Biblia. Kutaniko la Kikristo si chama cha kijamii au shirika la kilimwengu, lakini ni familia inayomwabudu Yehova Mungu kwa umoja. Tunawaita waamini wenzetu ndugu na dada kwa kuwa tunawaona kuwa washiriki wa familia yetu. Wao ni sehemu ya familia yetu ya kiroho, tunawapenda wakiwa marafiki wetu, na sikuzote tunawatendea kwa njia inayopatana na kanuni za Biblia. Acheni sote tuendelee kuchangia kifungo cha upendo ambacho kinaliunganisha na kulitambulisha kutaniko la kweli la Kikristo.—Yoh. 13:35.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 5 Neno a·gaʹpe linatumiwa pia kuhusiana na matendo yasiyofaa.—Yoh. 3:19; 12:43; 2 Tim. 4:10; 1 Yoh. 2:15-17.

^ fu. 7 Maneno “wasio na upendo wa asili” yametafsiriwa kutokana na aina fulani ya neno stor·geʹ ambalo lina maana isiyofaa, yaani, ‘kutokuwa na.’—Ona pia Waroma 1:31.

^ fu. 18 Katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, maneno mengine ya Kigiriki yanatafsiriwa pia kuwa “upendo mwororo.” Hivyo, katika tafsiri hiyo, maneno “upendo mwororo” yanapatikana katika Waroma 12:10, na pia katika Wafilipi 1:8, na 1 Wathesalonike 2:8.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Unachangia jinsi gani kifungo cha upendo kinachotuunganisha?