Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Mungu wa Upendo

Yehova Ni Mungu wa Upendo

“Mungu ni upendo.”—1 YOH. 4:8, 16.

NYIMBO: 18, 91

1. Mungu ana sifa gani kuu, na kujua sifa hiyo kunakufanya uhisije?

NENO la Mungu, Biblia, linatuambia kuwa “Mungu ni upendo.” Halisemi tu kwamba upendo ni kati ya sifa nzuri za Mungu, bali linasema, “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8) Upendo ndiyo sifa yake kuu. Si tu kwamba Yehova ana upendo, bali yeye ni upendo. Kwa kweli, tunafurahi sana kujua kwamba Muumba wa ulimwengu na vitu vyote ni Mungu wa upendo! Kila jambo analofanya linachochewa na sifa hiyo.

2. Upendo wa Mungu unatuhakikishia nini? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

2 Kwa kuwa Mungu anawapenda na kuwajali sana viumbe wake, tuna uhakika kwamba atatimiza kwa njia bora kabisa mambo yote ambayo amekusudia kuwafanyia wanadamu, na kuwanufaisha wale wote wanaokubali utawala wake. Kwa mfano, upendo umemchochea Yehova aweke “siku ambayo katika hiyo anakusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia kwa mwanamume ambaye amemweka rasmi,” Yesu Kristo. (Mdo. 17:31) Tuna uhakika kuwa hukumu hiyo itakuja, na hatimaye wanadamu wanyofu na watiifu watafurahia baraka za Yehova milele na milele.

HISTORIA INAONYESHA NINI?

3. Unafikiri maisha yangekuwaje ikiwa Mungu angekuwa hawapendi wanadamu?

3 Hebu wazia maisha yangekuwaje ikiwa Mungu angekuwa hawapendi wanadamu! Tungeendelea tu kushuhudia historia mbaya sana ya watawala wa ulimwengu huu walio chini ya mungu asiyejali na mwenye ghadhabu, Shetani Ibilisi. (2 Kor. 4:4; 1 Yoh. 5:19; soma Ufunuo 12:9, 12.) Jambo hilo linaonyesha kwamba wanadamu wangekuwa na hali mbaya sana wakati ujao ikiwa Mungu hangeupenda ulimwengu.

4. Kwa nini Yehova aliruhusu uasi dhidi ya utawala wake?

4 Ibilisi alipoasi utawala wa Yehova, aliwashawishi pia Adamu na Hawa wafanye vivyo hivyo. Alitilia shaka haki na uadilifu wa enzi kuu ya Mungu. Hivyo, Shetani alidai kwamba utawala wake ungekuwa bora kuliko utawala wa Mungu. (Mwa. 3:1-5) Yehova alimruhusu Shetani ajaribu kuthibitisha madai yake. Hata hivyo, ruhusa hiyo ni ya muda mfupi. Kwa kuwa Yehova ana hekima nyingi, aliamua kuacha wakati wa kutosha upite ili ionekane wazi kwamba yeye ndiye mtawala bora. Historia mbaya ya wanadamu inathibitisha kwamba wanadamu na Shetani hawawezi kamwe kuwa watawala wazuri.

5. Historia ya wanadamu inaonyesha nini?

5 Ndani ya miaka 100 iliyopita, zaidi ya watu milioni 100 wameuawa katika vita. Leo, hali za ulimwengu zinazidi kuwa mbaya. Neno la Mungu lilitabiri kwamba hali zingekuwa hivyo katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo, wakati ambapo “watu waovu na wajanja [wangeendelea] kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi.” (2 Tim. 3:1, 13) Historia inaonyesha wazi ukweli wa maneno haya ya Biblia: “Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yer. 10:23) Naam, wanadamu hawakuumbwa wakiwa na uwezo au haki ya kujiongoza bila msaada wa Yehova.

6. Uamuzi wa Mungu wa kuruhusu uovu unatoa uthibitisho gani?

6 Zaidi ya kuonyesha ubatili wa serikali za wanadamu, uamuzi wa Mungu wa kuruhusu uovu kwa muda mfupi unatimiza jambo lingine muhimu. Unatoa uthibitisho wa kudumu kwamba utawala wa Mungu pekee ndio unaoweza kufanikiwa. Wakati ujao, Yehova ataondoa uovu na kuwaharibu waovu. Baada ya hapo, ikiwa mtu yeyote atatilia shaka utawala wake wenye upendo, basi Mungu hatahitaji tena kuruhusu wakati upite ili kutatua suala hilo. Anaweza kutumia historia ya wanadamu kuwa msingi wa kuwaondoa mara moja waasi hao, na kutoruhusu tena uovu.

YEHOVA AMEONYESHAJE KWAMBA ANATUPENDA?

7, 8. Yehova ameonyeshaje kwamba anatupenda?

7 Kuna mambo mengi yanayothibitisha kwamba Yehova anawapenda viumbe wake. Kwa mfano, fikiria ulimwengu wetu maridadi. Kuna mabilioni ya makundi ya nyota, na kila kundi lina mabilioni ya nyota na sayari. Jua ni moja kati ya nyota zilizo kwenye kundi letu la Kilimia. Bila jua, kusingekuwa na kiumbe hai yeyote duniani. Uumbaji huo unathibitisha kwamba Yehova ndiye Mungu wetu na unafunua sifa zake, kama vile nguvu, hekima na upendo. Naam, “sifa [za Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea.”—Rom. 1:20.

8 Yehova aliumba kila kitu duniani kwa faida ya viumbe wake. Mungu aliwapa wanadamu bustani maridadi, naye aliwaumba wakiwa na akili kamilifu na mwili wenye uwezo wa kuishi milele. (Soma Ufunuo 4:11.) Isitoshe, Yehova huwapa “chakula wote wenye mwili: Kwa maana fadhili zake zenye upendo ni za mpaka wakati usio na kipimo.”—Zab. 136:25.

9. Yehova anachukia nini?

9 Yehova ni Mungu wa upendo, lakini anachukia mambo mabaya. Kwa mfano, Zaburi 5:4-6 inasema hivi kumhusu Yehova: “Wewe si Mungu anayependezwa na uovu . . . Wewe huwachukia wote wanaozoea kufanya mambo yenye kuumiza.” Kisha inaendelea kusema, “mtu anayemwaga damu na mdanganyifu Yehova anamchukia.”

UOVU UTAISHA HIVI KARIBUNI

10, 11. (a) Yehova atawafanya nini waovu? (b) Yehova atawathawabishaje wale wanaomtii?

10 Kwa kuwa Yehova ni Mungu wa upendo na anachukia uovu, anakusudia kuondoa kabisa uovu katika ulimwengu wote baada ya suala la enzi kuu kusuluhishwa kikamili. Neno la Mungu linaahidi hivi: “Watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia. Na bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena . . . Nao adui za Yehova watakuwa kama malisho bora; lazima wao waufikie mwisho wao. Katika moshi lazima waufikie mwisho wao.”—Zab. 37:9, 10, 20.

11 Kwa upande mwingine, Neno la Mungu linaahidi hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zab. 37:29) Watu hao waaminifu “watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” (Zab. 37:11) Tuna uhakika jambo hilo litatukia kwa sababu sikuzote Mungu wetu mwenye upendo anafanya mambo ambayo huwanufaisha watumishi wake waaminifu. Biblia inatuambia hivi: “Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufu. 21:4) Naam, wote wanaothamini kikweli upendo wa Yehova na kumtii watafurahia baraka nzuri ajabu!

12. “Mtu asiye na lawama” ni nani?

12 Neno la Yehova linasema hivi: “Mwangalie mtu asiye na lawama na uendelee kumwangalia mnyoofu, kwa maana wakati ujao wa mtu huyo utakuwa wenye amani. Lakini wakosaji hakika wataangamizwa pamoja; wakati ujao wa watu waovu hakika utakatiliwa mbali.” (Zab. 37:37, 38) “Mtu asiye na lawama” ni yule anayejifunza kumhusu Yehova na Mwana wake na kufanya mapenzi ya Mungu. (Soma Yohana 17:3.) Mtu huyo anazingatia maneno ya 1 Yohana 2:17: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” Mwisho wa ulimwengu unapozidi kukaribia, ni muhimu sana ‘tumtumaini Yehova na kuishika njia yake.’—Zab. 37:34.

UTHIBITISHO MKUBWA ZAIDI WA UPENDO WA MUNGU

13. Ni nini kinachothibitisha kwamba Yehova anatupenda sana?

13 Ingawa sisi si wakamilifu, tunaweza ‘kufuata njia ya Yehova.’ Dhabihu ya fidia ni uthibitisho mkubwa zaidi wa upendo wa Mungu, nayo inatuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Fidia ya Yesu Kristo inawaweka huru wanadamu watiifu kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo walichorithi kutoka kwa Adamu. (Soma Waroma 5:12; 6:23.) Yesu alikuwa mwaminifu kwa miaka mingi sana huko mbinguni, hivyo Yehova alikuwa na uhakika kabisa kwamba Mwana wake mzaliwa pekee angekuwa mwaminifu hapa duniani. Akiwa Baba mwenye upendo, bila shaka aliumia sana alipoona Yesu akitendewa kikatili alipokuwa duniani. Hata hivyo, Yesu alishikamana na enzi kuu ya Mungu na kuonyesha kwamba mwanadamu mkamilifu anaweza kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova hata anapokabili majaribu makali.

Mungu mwenye upendo alimtuma Mwana wake duniani, naye alikubali kwa hiari (Tazama fungu la 13)

14, 15. Kifo cha Yesu kina faida gani kwa wanadamu?

14 Licha ya kukabili majaribu makali, Yesu aliendelea kuwa mshikamanifu na aliunga mkono enzi kuu ya Yehova, naye akafa akiwa mwaminifu kwa Baba yake. Isitoshe, kupitia kifo chake, Yesu alilipa fidia iliyohitajika ili kuwakomboa wanadamu na kuwapa fursa ya kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. Mtume Paulo alisema hivi kuhusu upendo ambao Yehova na Yesu wameonyesha kupitia mpango wa fidia: “Kwa kweli, tulipokuwa tungali bado dhaifu, Kristo alikufa wakati uliowekwa kwa ajili ya watu wasiomwogopa Mungu. Kwa maana ni vigumu kwa yeyote kufa kwa ajili ya mtu mwadilifu; kwa kweli, labda, mtu anaweza kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu mwema. Lakini Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Rom. 5:6-8) Mtume Yohana aliandika hivi: “Kwa hili upendo wa Mungu ulifunuliwa kwa habari yetu, kwa sababu Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee kuja ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye. Hivi ndivyo upendo ulivyo, si kwamba sisi tumempenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda akamtuma Mwana wake kuwa dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu.”—1 Yoh. 4:9, 10.

15 Yesu alisema hivi kuhusu upendo wa Mungu: “Mungu aliupenda ulimwengu [wanadamu wanaoweza kukombolewa] sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Mungu anawapenda sana wanadamu hivi kwamba yuko tayari kuwafanyia mema haidhuru itamgharimu kadiri gani. Upendo wake ni wa milele. Hivyo, sikuzote tunaweza kumtumaini. Paulo aliandika hivi: “Nimesadiki kwamba wala kifo wala uzima wala malaika wala serikali wala mambo yaliyopo sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala uumbaji mwingine wowote havitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”—Rom. 8:38, 39.

UFALME WA MUNGU UNATAWALA SASA

16. Ufalme wa Kimasihi ni nini? Na Yehova amemchagua nani kuwa Mtawala wa Ufalme huo?

16 Ufalme wa Kimasihi, yaani, serikali ya Mungu, ni uthibitisho mwingine unaoonyesha kwamba Mungu anawapenda wanadamu. Tayari Yehova amekabidhi serikali hiyo mikononi mwa Mwana wake, ambaye anawapenda wanadamu na anastahili kabisa kutawala. (Met. 8:31) Baada ya kufufuliwa, wale 144,000 watakaotawala pamoja na Yesu mbinguni watakuwa watawala wazuri kwa kuwa wamewahi kuwa wanadamu. (Ufu. 14:1) Ufalme ndilo jambo kuu ambalo Yesu alifundisha, naye aliwaambia wanafunzi wake wasali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mt. 6:9, 10) Wanadamu watiifu watafurahia baraka nzuri ajabu Mungu atakapojibu sala zao!

17. Eleza tofauti iliyopo kati ya utawala wa Yesu na utawala wa wanadamu.

17 Kwa kweli, kuna tofauti kubwa kati ya utawala wenye upendo wa Yesu na utawala wa wanadamu ambao wamesababisha vifo vya mamilioni ya watu katika vita. Yesu anawajali kikweli raia wake na anaiga sifa nzuri za Mungu, hasa upendo. (Ufu. 7:10, 16, 17) Yesu alisema hivi: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:28-30) Maneno hayo yanatia moyo sana!

18. (a) Ufalme wa Mungu umefanya nini tangu ulipoanza kutawala? (b) Tutajibu maswali gani katika makala inayofuata?

18 Unabii wa Biblia unaonyesha kwamba Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mbinguni kuwapo kwa Kristo kulipoanza mwaka wa 1914. Tangu wakati huo, kumekuwa na kazi ya kukusanya idadi iliyobaki ya wale watakaotawala na Yesu mbinguni, na pia “umati mkubwa” wa watu watakaookoka mwisho wa mfumo huu na kuingia katika ulimwengu mpya. (Ufu. 7:9, 13, 14) Leo umati mkubwa una watu wengi kadiri gani? Na Mungu anataka wafanye nini? Tutajibu maswali hayo katika makala inayofuata.