Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Yesu Ni Mungu Mweza-Yote?

Je, Yesu Ni Mungu Mweza-Yote?

Je, Yesu Ni Mungu Mweza-Yote?

Watu wengi wanajibu hivi:

▪ “Ndiyo, Yesu ni Mungu Mweza-Yote.”

▪ “Yesu alikuwa Mungu katika mwili wa kibinadamu.”

Yesu alisema nini?

▪ “Kama mngenipenda, mngeshangilia kwamba ninaenda kwa Baba, kwa sababu Baba ni mkuu kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Yesu alisema kwamba yeye na Baba yake wana uwezo tofauti.

▪ “Mimi ninapanda kwenda kwa Baba yangu na Baba yenu na kwa Mungu wangu na Mungu wenu.” (Yohana 20:17) Yesu hakusema kwamba yeye ni Mungu bali alisema Mungu ni Mtu tofauti.

▪ “Sijasema kutokana na msukumo wangu mwenyewe, bali Baba mwenyewe aliyenituma amenipa amri kuhusu jambo la kutangaza na la kusema.” (Yohana 12:49) Yesu hakufundisha mambo yake mwenyewe; mafundisho yake yalitoka kwa Mungu.

YESU alisema yeye ni Mwana wa Mungu, si Mungu Mweza-Yote. Ikiwa Yesu alikuwa Mungu, alikuwa akisali kwa nani alipokuwa duniani? (Mathayo 14:23; 26:26-29) Bila shaka, halingekuwa jambo linalopatana na akili kwa Yesu kusingizia kuwa anazungumza na mtu mwingine!

Wanafunzi wawili wa Yesu walipomwomba awape vyeo vya pekee katika Ufalme wake, aliwajibu hivi: “Kuketi upande wangu wa kuume na upande wangu wa kushoto sina haki ya kutoa, bali wataketi wale ambao Baba yangu amewatayarishia.” (Mathayo 20:23) Je, Yesu alisema uwongo alipowaambia kwamba hakuwa na mamlaka ya kuwapa vyeo walivyotaka? Hakusema uwongo! Badala yake, kwa unyenyekevu alikubali kwamba ni Mungu peke yake aliyekuwa na mamlaka ya kufanya hivyo. Hata Yesu mwenyewe alisema kwamba kuna mambo ambayo yeye na malaika hawajui lakini ni Baba tu anayejua.—Marko 13:32.

Je, Yesu alikuwa na cheo cha chini kuliko Mungu wakati alipokuwa duniani tu? Hapana. Hata baada ya kufa na kufufuliwa, Biblia inasema kwamba Yesu aliendelea kuwa na cheo cha chini kuliko Mungu. Mtume Paulo anatukumbusha kwamba “kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Wakorintho 11:3) Biblia inasema kwamba wakati ujao “vitu vyote vitakapowekwa chini ya utawala wa Kristo, ndipo naye Mwana atakapojiweka chini ya Mungu, aliyeweka vyote chini ya utawala wake; ili Mungu atawale juu ya vyote.”—1 Wakorintho 15:28, Biblia Habari Njema.

Ni wazi kwamba Yesu si Mungu Mweza-Yote. Hiyo ndiyo sababu alimwita Baba yake “Mungu wangu.”—Ufunuo 3:2, 12; 2 Wakorintho 1:3, 4. *

[Maelezo ya chini]

^ fu. 12 Kwa habari zaidi kuhusu jambo hilo, ona ukurasa wa 201-204 katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Yesu alisema kwamba kuna mambo fulani ambayo yeye na malaika hawajui lakini ni Baba tu anayejua