Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuzaliwa Upya—Jinsi Gani?

Kuzaliwa Upya—Jinsi Gani?

Kuzaliwa Upya—Jinsi Gani?

YESU alizungumza na Nikodemo kuhusu umuhimu wa kuzaliwa upya, yule anayefanya mtu azaliwe upya, kusudi la kuzaliwa upya, na pia jinsi mtu anavyozaliwa upya. Yesu alisema: “Mtu asipozaliwa kwa maji na roho, hawezi kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Yohana 3:5) Hivyo, mtu anazaliwa tena kwa maji na roho. Lakini maneno “maji na roho” yanarejelea nini?

Maana ya “Maji na Roho”

Kwa kuwa Nikodemo alikuwa msomi wa Dini ya Kiyahudi, hapana shaka alijua jinsi Maandiko ya Kiebrania yanavyotumia maneno “roho ya Mungu”—nguvu za utendaji za Mungu zinazoweza kuwafanya watu watende maajabu. (Mwanzo 41:38; Kutoka 31:3; 1 Samweli 10:6) Kwa hiyo, Yesu alipotumia neno “roho,” Nikodemo alielewa kwamba alimaanisha roho takatifu, yaani, nguvu za utendaji za Mungu.

Yesu alimaanisha nini alipotaja maji? Angalia matukio yanayotangulia na yanayofuata mazungumzo ya Yesu na Nikodemo. Yanaonyesha kwamba Yohana Mbatizaji na wanafunzi wa Yesu walibatiza kwa maji. (Yohana 1:19, 31; 3:22; 4:1-3) Ubatizo huo ulijulikana sana huko Yerusalemu. Kwa hiyo, Yesu alipotaja maji, Nikodemo alitambua kwamba alikuwa akizungumza kuhusu maji ya ubatizo bali si maji tu kwa ujumla. *

Kubatizwa “kwa Roho Takatifu”

Ikiwa “kuzaliwa kwa maji” kunahusiana na kubatizwa kwa maji, ‘kuzaliwa kwa roho’ kunamaanisha nini? Kabla ya mazungumzo ya Nikodemo na Yesu, Yohana Mbatizaji alikuwa ametangaza kwamba maji na pia roho ingetumika katika kubatiza. Alisema: “Mimi niliwabatiza ninyi kwa maji, lakini yeye [Yesu] atawabatiza ninyi kwa roho takatifu.” (Marko 1:7, 8) Mwandikaji wa Injili anayeitwa Marko anataja wakati wa kwanza ambapo ubatizo wa aina hiyo ulifanywa. Anaandika: “Baada ya siku hizo Yesu akaja kutoka Nazareti ya Galilaya, Yohana akambatiza katika Yordani. Mara moja alipopanda kutoka majini akaona mbingu zikifunguka, na roho ikashuka juu yake kama njiwa.” (Marko 1:9, 10) Yesu alipozamishwa katika Mto Yordani, alibatizwa kwa maji. Mara alipopokea roho kutoka mbinguni, alibatizwa kwa roho takatifu.

Miaka mitatu hivi baada ya kubatizwa, Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake hivi: “Ninyi mtabatizwa kwa roho takatifu siku chache baadaye.” (Matendo 1:5) Walibatizwa kwa roho wakati gani?

Siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., wanafunzi wa Yesu wapatao 120 walikuwa wamekusanyika katika nyumba fulani huko Yerusalemu. “Ghafula kukatokea kutoka mbinguni kelele kama ile ya upepo wenye nguvu unaovuma, nao ukaijaza nyumba yote ambamo walikuwa wameketi. Nao wakaona ndimi kama za moto . . . , nao wote wakajazwa roho takatifu.” (Matendo 2:1-4) Siku hiyohiyo, watu wengine huko Yerusalemu walihimizwa wabatizwe kwa maji. Mtume Petro aliuambia umati hivi: “Tubuni, na acheni kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo kwa msamaha wa dhambi zenu, nanyi mtapokea zawadi ya bure ya roho takatifu.” Watu hao walifanya nini? “Wale waliokubali neno lake kwa ukunjufu wa moyo wakabatizwa, na katika siku hiyo nafsi karibu elfu tatu zikaongezwa.”—Matendo 2:38, 41.

Kubatizwa kwa Njia Mbili

Ubatizo wa maji na wa roho takatifu unafunua nini kuhusu kuzaliwa upya? Unaonyesha kwamba mtu anahitaji kubatizwa kwa njia mbili ili azaliwe upya. Ona kwamba Yesu alibatizwa kwanza kwa maji. Kisha akapokea roho takatifu. Vivyo hivyo, wanafunzi wa kwanza walibatizwa kwanza kwa maji (baadhi yao na Yohana Mbatizaji), kisha wakapokea roho takatifu. (Yohana 1:26-36) Pia, wale wanafunzi wapya 3,000 walibatizwa kwanza kwa maji, kisha wakapokea roho takatifu.

Tunapozingatia kwamba wanafunzi wapya walibatizwa kwa njia mbili siku ya Pentekoste 33 W.K., tutatarajia mtu azaliwe upya kwa njia gani leo? Katika njia ileile ambayo mitume wa Yesu na wanafunzi wake wa kwanza walizaliwa upya. Kwanza mtu anatubu dhambi zake, anageuka na kuacha mwenendo mbaya, anajiweka wakfu kwa Yehova ili kumwabudu na kumtumikia, na kuonyesha hadharani kwamba amejiweka wakfu kwa kubatizwa kwa maji. Kisha, Mungu akimchagua kuwa mtawala katika Ufalme Wake, anamtia mafuta kwa roho takatifu. Mtu mwenyewe ndiye anayechukua hatua ya kwanza ya kubatizwa kwa maji, lakini Mungu ndiye anayechukua hatua ya pili ya kumbatiza kwa roho. Hivyo, mtu anazaliwa upya anapobatizwa katika njia zote mbili.

Lakini kwa nini Yesu alitumia maneno ‘kuzaliwa kwa maji na roho’ alipozungumza na Nikodemo? Alikuwa akikazia kwamba hali ya wale wanaobatizwa kwa maji na kwa roho inabadilika sana. Habari inayofuata inazungumzia badiliko hilo linalotokana na kuzaliwa upya.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 5 Vivyo hivyo, pindi moja mtume Petro alisema hivi kuhusu watu waliotaka kubatizwa: “Je, mtu yeyote anaweza kuyakataza maji?”—Matendo 10:47.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yohana aliwabatiza kwa maji Waisraeli waliotubu