Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, ukuta wa miti iliyochongoka ulijengwa kuzunguka Yerusalemu kama Yesu alivyotabiri?

Katika unabii wake kuhusu uharibifu wa Yerusalemu, Yesu alisema hivi: “Siku zitakuja juu yako wakati adui zako watakapojenga kukuzunguka ngome yenye miti iliyochongoka nao watakuzunguka na kukutaabisha kutoka kila upande.” (Luka 19:43) Maneno ya Yesu yalitimia mwaka wa 70 W.K., wakati ambapo Waroma walioongozwa na Tito walijenga ukuta uliozunguka Yerusalemu. Kusudi la Tito lilikuwa kuwazuia Wayahudi wasikimbie Yerusalemu ili kuwalazimisha wajisalimishe, na kama hilo halingefaulu, kusababisha njaa ili wasalimu amri.

Mwanahistoria wa karne ya kwanza anayeitwa Flavio Yosefo anasema kwamba mara Tito alipoamua kujenga ukuta huo, vikosi na vikundi vingine vidogo vya jeshi la Waroma walishindana kujenga sehemu za ukuta walizogawiwa kujenga. Miti yote ilikatwa kufikia umbali wa kilomita 16 hivi pande zote za Yerusalemu. Ilichukua siku tatu tu kujenga ukuta huo wenye urefu wa kilomita saba hivi. Yosefo anasema kwamba baada ya ukuta huo kujengwa, “Wayahudi hawakuwa na njia yoyote ya kutorokea.” Kwa sababu ya ukuta huo, njaa ilikumba Yerusalemu, na vikundi mbalimbali vya watu wenye silaha wakaanza kupigana na kuuana jijini humo. Yapata miezi mitano baadaye, jiji hilo lilitekwa na Waroma.

Je, Mfalme Hezekia alijenga mfereji wa chini kwa chini?

Hezekia alikuwa mfalme wa Yuda mwishoni mwa miaka ya 700 K.W.K. Hizo zilikuwa nyakati za vita kati ya Yuda na Milki ya Ashuru yenye nguvu. Biblia inatuambia kwamba Hezekia alifanya mengi ili kulinda Yerusalemu na kuhakikisha kwamba jiji hilo lingekuwa na maji nyakati za vita. Mojawapo ya mambo aliyofanya ni kujenga mfereji wa chini kwa chini wenye urefu wa mita 533, ili kuleta maji ya chemchemi jijini humo.—2 Wafalme 20:20; 2 Mambo ya Nyakati 32:1-7, 30.

Mfereji kama huo uligunduliwa katika miaka ya 1800, nao ulikuja kuitwa Mfereji wa Hezekia, au Mfereji wa Siloamu. Ndani ya mfereji huo kuna maandishi yanayoeleza kuhusu ujenzi wa sehemu ya mwisho ya mfereji. Kwa sababu ya umbo la herufi za maandishi hayo, wasomi wengi wanakadiria kwamba mfereji huo ulijengwa katika siku za Hezekia. Hata hivyo, miaka kumi iliyopita, baadhi ya wasomi walidai kwamba mfereji huo ulijengwa miaka 500 hivi baadaye. Mwaka wa 2003, kikundi cha wanasayansi Waisraeli walichapisha matokeo ya uchunguzi wao uliofanywa ili kuthibitisha wakati ambapo mfereji huo ulijengwa. Walikata kauli gani?

Dakt. Amos Frumkin wa chuo kikuu fulani huko Yerusalemu anasema hivi: “Kwa kupima mnururisho wa kaboni-14 katika lipu iliyo ndani ya mfereji huu, na kwa kupima mnururisho . . . katika mawe ya chokaa yanayopatikana humo, tumethibitisha kabisa kwamba Mfereji wa Siloamu ulijengwa katika siku za Hezekia.” Makala moja katika jarida la Nature inaongeza hivi: “Njia hizi tatu za kuthibitisha mambo—upimaji wa mnururisho, uchunguzi wa maandishi, na historia—zote zinaonyesha kwamba Mfereji wa Siloamu ulijengwa mwaka wa 700 hivi kabla ya Kristo. Hivyo, wakati wa kujengwa kwa mfereji huo umethibitishwa vizuri zaidi kuliko wakati wa ujenzi mwingine wowote katika Enzi ya Chuma unaotajwa katika Biblia.”