Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dini Zote Zinaelekeza Watu kwa Mungu Yuleyule?

Je, Dini Zote Zinaelekeza Watu kwa Mungu Yuleyule?

Je, Dini Zote Zinaelekeza Watu kwa Mungu Yuleyule?

“Mimi nina dini yangu mwenyewe, na siwezi kuiacha. Isitoshe, dini si hoja, kwa kuwa dini zote zinaelekeza watu kwa Mungu yuleyule.”

JE, UMEWAHI kumsikia mtu akisema hivyo? Watu wengi wanaamini kwamba dini yoyote inaweza kumsaidia mtu kumjua Mungu na kuelewa maana ya maisha. Vivyo hivyo, wengine wanaamini kwamba kila dini ina ubaya na uzuri wake, na kwamba hakuna dini inayoweza kudai kuwa hiyo tu ndiyo ya kweli au ndiyo inayoelekeza watu kwa Mungu.

Maoni hayo yameenea sana kati ya watu wanaodai kwamba hawapingi imani za wengine na wanaofikiri dini zote ni sawa. Mara nyingi wale walio na msimamo tofauti wanaonwa kuwa wenye maoni finyu, au wenye imani kali. Una maoni gani? Je, unafikiri kwamba dini zote zinaelekeza watu kwa Mungu yuleyule? Je, ni sawa tu hata kama mtu anafuata dini gani?

Je, Kweli Mafundisho ya Dini Yanapatana?

Ensaiklopidia moja inasema kwamba sasa kuna dini 9,900 duniani. Baadhi ya dini hizo zimesambaa sehemu nyingi ulimwenguni na zina mamilioni ya wafuasi. Inakadiriwa kwamba asilimia 70 ya wanadamu ni wafuasi wa dini tano kubwa ambazo ni dini ya Kiyahudi, Ubudha, Uhindu, Uislamu, na Ukristo. Ikiwa dini zote zinaelekeza watu kwa Mungu yuleyule, bila shaka dini hizo tano zinapaswa kuwa na mambo mengi yanayopatana katika mafundisho yao, na ufafanuzi wao kumhusu Mungu na kusudi lake. Lakini ukweli ni nini?

Hans Küng, mwanatheolojia wa Kanisa Katoliki, anasema kwamba dini kubwa zinapatana katika mafundisho fulani ya msingi kuhusu jinsi watu wanavyopaswa kutendeana. Kwa mfano, dini nyingi zinapinga kuua, kusema uwongo, kuiba, na kufanya ngono na mtu wa ukoo, na zinafundisha kwamba watoto wanapaswa kuwaheshimu wazazi, nao wazazi wanapaswa kuwapenda watoto wao. Lakini katika mambo mengine, na hasa ufafanuzi wao kumhusu Mungu, dini hizo kubwa hazipatani hata kidogo.

Kwa mfano, Wahindu wanaabudu miungu mingi sana, na inasemekana kuwa Wabudha hawana uhakika kwamba Mungu ni halisi. Waislamu wanafundisha kwamba Mungu ni mmoja na ndivyo na makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo. Hata hivyo, mengi ya makanisa hayo yanadai pia kwamba Mungu ni Utatu. Isitoshe, makanisa hayo yanafundisha mambo mengi yanayotofautiana. Wakatoliki wanamtukuza Maria, mama ya Yesu, katika ibada yao, lakini Waprotestanti hawafanyi hivyo. Kwa jumla, Wakatoliki wanakatazwa kutumia njia za kuzuia kupata mimba lakini Waprotestanti wengi hawakatazwi. Waprotestanti hawakubaliani ikiwa ni sawa au si sawa kwa watu wa jinsia moja kufanya ngono.

Je, ni jambo linalopatana na akili kufikiri kwamba wafuasi wa dini hizo zote zinazofundisha mambo ambayo yanatofautiana kadiri hiyo, wanaweza kuwa wanamwabudu Mungu yuleyule? Hapana. Kinyume chake, watu hao wanaweza tu kuchanganyikiwa wasijue ukweli kumhusu Mungu na jinsi anavyotaka aabudiwe.

Dini Zinaunganisha Watu au Zinawagawanya?

Ikiwa dini zote zinaelekeza watu kwa Mungu yuleyule, bila shaka tungeona kila moja ikijitahidi sana kuunganisha watu wawe na amani. Je, mambo ya hakika yanathibitisha wanafanya hivyo? Historia inaonyesha kwamba badala ya dini kuunganisha wanadamu inasababisha mgawanyiko na vita. Hebu tuone mifano kadhaa.

Kuanzia karne ya 11 hadi ya 13, mataifa yanayodai kuwa ya Kikristo yalipigana na serikali za Kiislamu katika vita mbalimbali vya dini. Katika karne ya 17 Wakatoliki na Waprotestanti walipigana katika vile Vita vya Miaka 30. Mwaka wa 1947, mara tu Uingereza ilipozipa uhuru nchi za bara Hindi, Wahindu na Waislamu walianza kupigana. Hivi karibuni, Wakatoliki na Waprotestanti wamepigana kwa miaka mingi huko Ireland Kaskazini. Huko Mashariki ya Kati, Wayahudi na Waislamu hawaishi kwa amani. Isitoshe, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipiganwa na dini zote tano kubwa, hata wafuasi wa dini ileile walipigana wakiwa pande tofauti za majeshi ya nchi zilizokuwa zikipigana

Mambo hayo yanaonyesha waziwazi kwamba dini za ulimwengu zimeshindwa kuleta amani na umoja. Pia zimeshindwa kuwaelekeza wanadamu kwa Mungu yuleyule. Badala yake, zimewagawanya na kuwachanganya wasielewe ukweli kumhusu Mungu na jinsi ya kumwabudu. Kwa hiyo, lazima yeyote anayetaka kuwa na uhusiano na Mungu wa kweli achague kwa uangalifu njia atakayofuata. Hilo linapatana na shauri la Biblia, ambayo ni kitabu cha dini cha kale zaidi kinachojulikana na wanadamu.

Jichagulieni Yule Mtakayemtumikia

Biblia inaonyesha wazi kwamba ili kuipata njia itakayokuelekeza kwa Mungu unahitaji kufikiria kwa makini na kufanya uamuzi kwa uangalifu. Yoshua, mtumishi wa Yehova Mungu, aliliambia hivi taifa la kale la Israeli: “Jichagulieni leo yule mtakayemtumikia, kama ni miungu ambayo waliitumikia mababu zenu waliokuwa ng’ambo ile nyingine ya Mto au kama ni miungu ya Waamori ambao mnakaa katika nchi yao. Lakini mimi na nyumba yangu, tutamtumikia Yehova.” Miaka mingi baadaye, nabii Eliya aliwahimiza watu wafanye uamuzi kama huo aliposema: “Mtayumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti mpaka wakati gani? Ikiwa Yehova ndiye Mungu wa kweli, mfuateni yeye; lakini ikiwa ni Baali [mungu wa Wakanaani], mfuateni yeye.”—Yoshua 24:15, 16; 1 Wafalme 18:21.

Maandiko hayo na mengineyo yanaonyesha waziwazi kwamba wale waliotaka kumtumikia Mungu wa kweli walihitaji kufanya uamuzi kwa uangalifu. Ndivyo ilivyo leo. Ikiwa tunataka kumtumikia Mungu wa kweli, lazima tufanye uamuzi unaofaa. Lakini ni nini kinachoweza kutusaidia kufanya uamuzi huo kuhusu ibada? Tunaweza kuwatambua waabudu wa kweli jinsi gani?

Waabudu wa Kweli Wanatambuliwa kwa Matunda Yao

Kuhusu waabudu wa kweli na wa uwongo, Yesu Kristo aliwaambia wafuasi wake: “Je, watu hukusanya zabibu kutoka kwenye miiba au tini kutoka kwenye michongoma? Vivyo hivyo kila mti mzuri huzaa matunda mazuri, lakini kila mti uliooza huzaa matunda yasiyofaa; mti mzuri hauwezi kuzaa matunda yasiyofaa, wala mti uliooza hauwezi kuzaa matunda mazuri. . . . Basi, kwa kweli kwa matunda yao mtawatambua watu hao.” Kwa hiyo, waabudu wa kweli wangetambuliwa kwa matunda yao, au matendo. Matunda hayo ni gani?—Mathayo 7:16-20.

Kwanza, ibada ya kweli inawaunganisha waamini katika upendo. Yesu aliwaeleza wanafunzi wake: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” Lazima wafuasi wa kweli wa Kristo wapendane kwa njia inayowatambulisha waziwazi mbele ya watu kwamba wao ni waabudu wa kweli.—Yohana 13:34, 35.

Kwa sababu hiyo, Wakristo wa kweli hawapaswi kamwe kupigana wao kwa wao vitani. Je, wafuasi wa dini nyingine wanafuata kanuni hiyo? Katika Vita vya Pili vya Ulimwengu, ni Mashahidi wa Yehova pekee waliokataa katakata kuunga mkono vita. Dakt. Hanns Lilje, aliyekuwa askofu wa Kanisa la Kiprotestanti jijini Hannover, Ujerumani, aliandika hivi kuwahusu Mashahidi: “Wana haki ya kusema kwamba wao ndio kikundi kikubwa cha dini ambacho, kwa sababu ya dhamiri, kilikataa kujiunga na vita wakati wa utawala wa Nazi.” Wakati wa vita hivyo, Mashahidi katika nchi nyingi waliamua ni heri kuteswa kuliko kuunga mkono vita.

Ni matunda gani mengine ambayo Yesu alikuwa akifikiria ambayo yangewatambulisha wanafunzi wa kweli? Katika ile sala ambayo kwa kawaida inaitwa Sala ya Bwana, Yesu alianza kwa kusema: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” Yesu anataja kwanza kutakaswa kwa jina la kibinafsi la Mungu, ambalo ni Yehova. Kisha anaomba mapenzi ya Yehova yatimizwe duniani kupitia Ufalme wa Mungu. Ni dini gani ambayo inajulikana kwa kutangaza jina la Yehova na Ufalme wake ambao ndio tu unaoweza kuleta amani duniani? Mashahidi wa Yehova wanatangaza habari njema ya Ufalme katika nchi na maeneo 236 na kugawa vichapo katika lugha zaidi ya 470.—Mathayo 6:9, 10.

Isitoshe, Mashahidi wa Yehova wanafuata mfano wa Yesu kwa kuepuka mabishano ya kisiasa au ya kijamii. Yesu alisema hivi kuwahusu wanafunzi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” Pia, Mashahidi wanaikubali Biblia kuwa Neno la Mungu na wana uhakika kwamba “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—Yohana 17:14, 17; 2 Timotheo 3:16, 17.

Dini ya Kweli Ni Tofauti

Matunda haya—upendo wa kujidhabihu, tamaa ya kulitakasa jina la Yehova, kutangaza Ufalme wa Mungu, kujitenga na ulimwengu, na kuiamini Biblia—yote yanawatambulisha waabudu wa kweli. Matunda hayo pia yanaonyesha tofauti kati ya waabudu wa kweli na dini nyingine. Mwanamke mmoja aliyezungumza na Mashahidi wa Yehova mara kadhaa alifikia uamuzi huu: “Ninajua dini nyingi, na zote zinafanana. Nyinyi tu ndio mlio tofauti kabisa na wengine.”

Kwa hiyo, ni wazi kwamba dini zote hazielekezi watu kwa Mungu yuleyule. Lakini kuna kikundi kimoja ambacho ni tofauti na vingine—Mashahidi wa Yehova, ambao idadi yao sasa ni zaidi ya milioni saba ulimwenguni. Kwa kulitangaza na kulitii Neno la Mungu, Biblia, wametimiza jambo ambalo hakuna kikundi au shirika lingine limeweza kutimiza, yaani, kuwaunganisha watu wa mataifa, lugha, kabila, na jamii mbalimbali kumwabudu Mungu mmoja wa kweli, Yehova. Watafurahi kukusaidia kujifunza kumhusu Mungu wa kweli, kujua mambo anayotaka ufanye, na kufurahia amani na usalama unaotokana na kumwabudu Mungu katika njia anayokubali. Huo ni mradi unaofaa kama nini!

[Picha katika ukurasa wa 14]

Kasisi wa Kanisa Othodoksi akibariki kikosi kipya cha jeshi nchini Ukrainia mwaka wa 2004

[Hisani]

GENIA SAVILOV/AFP/Getty Images

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mashahidi wa Yehova wanawasaidia watu kila mahali wajifunze kumhusu Mungu na Ufalme wake

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 12]

Page 12: Buddhist woman: © Yan Liao/Alamy; Hindu holy man: © imagebroker/Alamy; page 13: Man reading Koran: Mohamed Amin/Camerapix; Jewish man: Todd Bolen/Bible Places.com