Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwamuzi Anayehukumu kwa Haki

Mwamuzi Anayehukumu kwa Haki

Mkaribie Mungu

Mwamuzi Anayehukumu kwa Haki

Hesabu 20:2-13

MAHAKIMU wa kibinadamu wanaweza kutoa hukumu isiyofaa au ambayo ni kali kupita kiasi, lakini Yehova Mungu hawezi kufanya hivyo kwa kuwa yeye ni “mpenda-haki.” (Zaburi 37:28) Ingawa yeye ni mwenye subira, hawaendekezi watu. Anashikamana na yaliyo sawa. Fikiria jinsi alivyotenda Waisraeli walipomnung’unikia na kuasi, kama ilivyorekodiwa kwenye Hesabu sura ya 20.

Walipokuwa karibu kumaliza safari nyikani, Waisraeli walikabili tatizo la upungufu wa maji. * Watu walianza kubishana na Musa na Haruni wakisema: “Kwa nini ninyi mmeleta kutaniko la Yehova katika nyika hii ili sisi na wanyama wetu wa kubeba mizigo tufie huko?” (Mstari wa 4) Watu walilalamika kwamba nyika ilikuwa ‘mahali pabaya’ ambapo hapakuwa na “tini na mizabibu na makomamanga”—tunda ambalo wapelelezi Waisraeli walileta kutoka kwenye Nchi ya Ahadi miaka kadhaa mapema—na kwamba hapakuwa na “maji ya kunywa.” (Mstari wa 5; Hesabu 13:23) Kwa kweli, walikuwa wakiwalaumu Musa na Haruni kwa sababu nyika hiyo haikuwa kama nchi yenye rutuba ambayo kizazi kilichotangulia cha wanung’unikaji kilikuwa kimekataa kuiingia!

Yehova hakupuuza manung’uniko yao. Badala yake, alimwambia Musa afanye mambo matatu: achukue fimbo yake, awakusanye watu, na ‘kuuambia mwamba mbele ya macho yao ili kwa kweli utoe maji yake.’ (Mstari wa 8) Musa alitii mambo mawili ya kwanza, lakini hakutii jambo la tatu. Badala ya kuzungumza na mwamba kwa imani, alizungumza na watu kwa uchungu akisema: “Sikieni, sasa, enyi waasi! Je, tuwatolee ninyi maji katika mwamba huu?” (Mstari wa 10; Zaburi 106:32, 33) Kisha Musa akaupiga mwamba mara mbili, “na maji mengi yakaanza kutoka.”—Mstari wa 11.

Kwa sababu hiyo, Musa, pamoja na Haruni, wakafanya dhambi nzito. “Ninyi mliasi agizo langu,” Mungu akawaambia. (Hesabu 20:24) Pindi hii walipotenda kinyume cha agizo la Mungu, Musa na Haruni wakawa kile walichowaita watu wale wengine, yaani, wakawa waasi. Hukumu ya Mungu ilikuwa wazi: Musa na Haruni hawangewaongoza Waisraeli kuingia kwenye Nchi ya Ahadi. Je, hukumu hiyo ilikuwa kali kupita kiasi? Hapana; kwa sababu kadhaa.

Kwanza, Mungu hakumwagiza Musa azungumze na watu, sembuse kuwahukumu kuwa waasi. Pili, Musa na Haruni hawakumpa Mungu utukufu. ‘Hamkunitakasa,’ Mungu akasema. (Mstari wa 12) Kwa kusema “tuwatolee ninyi maji,” Musa alizungumza kana kwamba yeye na Haruni—si Mungu—ndio waliokuwa wakiwaandalia maji hayo kimuujiza. Tatu, hukumu hiyo ililingana na hukumu zilizokuwa zimetolewa awali. Mungu hakuwaruhusu waasi wa kizazi kilichotangulia waingie Kanaani, kwa hiyo hakuwaruhusu Musa na Haruni pia waingie. (Hesabu 14:22, 23) Nne, Musa na Haruni walikuwa viongozi wa Israeli. Wale walio na madaraka mengi wanawajibika zaidi kwa Mungu.—Luka 12:48.

Yehova anashikamana na yaliyo sawa. Kwa sababu anapenda haki, hawezi kutoa hukumu ambazo si za haki. Kwa kweli, tunastahili kumtegemea na kumheshimu Mwamuzi kama huyo.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 2 Baada ya kutoka Misri, Waisraeli walikuwa tayari kuingia Kanaani, nchi ambayo Mungu alikuwa amemwahidi Abrahamu. Lakini wapelelezi kumi walipoleta ripoti mbaya, watu walianza kunung’unika dhidi ya Musa. Kwa hiyo, Yehova alisema kwamba walipaswa kukaa nyikani kwa miaka 40—muda wa kutosha kwa kizazi hicho kilichoasi kufa.