Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Roho Takatifu—Nguvu Unayohitaji Maishani

Roho Takatifu—Nguvu Unayohitaji Maishani

Roho Takatifu—Nguvu Unayohitaji Maishani

“USINITUPILIE mbali na uso wako; wala usiniondolee roho yako takatifu.” (Zaburi 51:11) Hiyo ilikuwa sala ya kutoka moyoni ya Mfalme Daudi baada ya kufanya kosa zito sana.

Daudi aliona mara nyingi roho takatifu ikitenda katika maisha yake. Alipokuwa bado kijana, roho hiyo ilimwezesha kumwangamiza Goliathi, askari-jeshi mwenye kutisha. (1 Samweli 17:45-50) Pia, ilimpa nguvu za kuandika baadhi ya zaburi maridadi kuwahi kutungwa. Daudi alisema hivi: “Roho ya Yehova ndiyo iliyosema kupitia mimi, na neno lake lilikuwa kwenye ulimi wangu.”—2 Samweli 23:2.

Yesu Kristo mwenyewe alithibitisha kwamba roho takatifu ilitimiza fungu fulani katika maisha ya Daudi. Pindi moja Yesu aliwaambia hivi wasikilizaji wake: “Kwa roho takatifu Daudi mwenyewe alisema, ‘Yehova alimwambia Bwana wangu: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke adui zako chini ya miguu yako.”’” (Marko 12:36; Zaburi 110:1) Yesu alijua kwamba Daudi alipoandika Zaburi zake, aliongozwa na roho takatifu. Je, roho hiyohiyo takatifu inaweza kutusaidia?

“Endeleeni Kuomba, Nanyi Mtapewa”

Huenda hutawahi kuandika zaburi. Lakini huenda ukakabili matatizo makubwa yaliyo kama Goliathi yenye kukatisha tamaa. Kwa mfano, mfikirie Isabel. * Mume wake alimwacha ili akaishi na msichana fulani. Alimwachia madeni chungu nzima, na hakumsaidia kifedha kuwatunza binti zao wawili. “Nilijihisi nikiwa nimesalitiwa na kutendewa kama takataka,” anasema. “Hata hivyo, tangu aniache, nimeona kwamba roho takatifu ya Mungu imenitegemeza.”

Je, Isabel alitarajia kupata roho takatifu pasipo jitihada zozote? Hapana, kila siku alimsihi Mungu ampe roho yake. Alijua kwamba alihitaji nguvu za Mungu ili aweze kukabiliana na wakati ujao kwa ujasiri, kutunza watoto wake vizuri, na kujiheshimu tena. Alifuata maneno haya ya Yesu: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa.”—Mathayo 7:7.

Pia, Roberto alihisi kwamba anahitaji roho ya Mungu lakini kwa sababu tofauti. Alikuwa mraibu wa tumbaku na bangi, ambazo alikuwa akivuta kwa ukawaida. Kwa miaka miwili alijaribu kuacha uraibu wake lakini alirudia zoea hilo mara kadhaa. Roberto anasema hivi: “Unavurugikiwa sana unapoacha kutumia dawa za kulevya. Mwili huendelea kudai dawa hizo kila siku.”

Roberto anaendelea kusema: “Lakini nilikuwa nimeazimia kubadili maisha yangu ili nimtumikie Mungu kwa njia inayokubalika. Nilijaribu kuijaza akili yangu mambo yanayofaa kutoka katika Biblia. Nilisali kwa bidii kila siku, nikimwomba Mungu anipe nguvu za kurekebisha maisha yangu. Nilijua kwamba siwezi kufaulu kwa nguvu zangu mwenyewe. Niliona jinsi Yehova alivyojibu sala zangu, hasa nilipohisi nimevunjika moyo baada ya kurudia tena uraibu wangu. Ninaamini kwamba roho takatifu ya Mungu ilinipa nguvu mpya; bila roho yake singeweza kuushinda uraibu wangu.”—Wafilipi 4:6-8.

Kuruka Juu “kwa Mabawa Kama Tai”

Kama tu Isabel na Roberto, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wameona nguvu za roho takatifu zikitenda katika maisha yao. Unaweza kupata nguvu za utendaji za Yehova, ambazo pia zilitumiwa katika uumbaji wa ulimwengu. Mungu yuko tayari na anatamani sana kukupa roho yake ikiwa utamwomba kwa bidii. Lakini ili upate roho hiyo, unahitaji kujifunza kweli kumhusu na kufanya mapenzi yake kwa unyoofu.—Isaya 55:6; Waebrania 11:6.

Kupitia nguvu za roho takatifu, unaweza kuimarishwa kumtumikia Mungu kwa mafanikio na kukabiliana na magumu yoyote yanayoweza kutokea maishani mwako. Biblia inatuhakikishia hivi: “[Yehova] anampa nguvu mtu aliyechoka; naye huzijaza nguvu kamili kwa mtu asiye na nguvu zenye msukumo. . . . Wale wanaomtumaini Yehova watapata nguvu mpya. Wataruka juu kwa mabawa kama tai. Watakimbia wala hawatazimia; watatembea wala hawatachoka.”—Isaya 40:28-31.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 6 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

‘Nilisali kwa bidii kila siku, nikimwomba Mungu anipe nguvu. Nilijua kwamba siwezi kufaulu kwa nguvu zangu mwenyewe. Niliona jinsi Yehova alivyojibu sala zangu’

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

UTENDAJI WA ROHO TAKATIFU

Mungu alitumia roho takatifu kuumba dunia na ulimwengu wote. “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima. Dunia imejaa vitu ulivyotokeza,” akasema mtunga-zaburi. “Ukiituma roho yako, wanaumbwa.”—Zaburi 104:24, 30; Mwanzo 1:2; Ayubu 33:4.

Roho takatifu iliwaongoza wanaume wanaompenda Mungu kuiandika Biblia. “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa,” akaandika mtume Paulo. (2 Timotheo 3:16, Union Version) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “pumzi ya Mungu” kihalisi linamaanisha “kupuliziwa na Mungu.” Pumzi, au roho ya Yehova, iliongoza fikira za waandikaji wa Biblia, kwa hiyo waliwasilisha “neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.

Roho takatifu iliwapa watumishi wa Mungu nguvu za kutabiri wakati ujao kwa usahihi. Mtume Petro alieleza hivi: “Hakuna unabii wa Andiko unaotokana na fasiri yoyote ya kibinafsi. Kwa maana unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.”—2 Petro 1:20, 21; Yoeli 2:28.

Roho takatifu ilimsaidia Yesu na wanaume wengine wenye imani wahubiri kuhusu habari njema ya Ufalme wa Mungu na kufanya miujiza. Yesu alisema: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kuwatangazia maskini habari njema, alinituma kuhubiri kuachiliwa huru kwa mateka na kupata kuona tena kwa vipofu.”—Luka 4:18; Mathayo 12:28.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

NJIA AMBAZO ROHO TAKATIFU INAWEZA KUTUSAIDIA

Roho takatifu inaweza kukuimarisha ukabiliane na vishawishi na ushinde mazoea yenye kudhuru. Mtume Paulo alisema: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.”—1 Wakorintho 10:13.

Roho takatifu inaweza kukusaidia kusitawisha sifa za kimungu. “Matunda ya roho ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.”—Wagalatia 5:22, 23.

Roho takatifu inaweza kukuimarisha kuvumilia majaribu. “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”—Wafilipi 4:13.