Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni ya Mungu Kuhusu Pombe

Maoni ya Mungu Kuhusu Pombe

Maoni ya Mungu Kuhusu Pombe

MUUMBA wetu, anayetaka tuwe na maisha bora, hatukatazi kunywa pombe kwa kiasi. * Amempa mwanadamu “divai ya kumchangamsha, mafuta ya zeituni ya kumfurahisha, na mkate wa kumpa nguvu.” (Zaburi 104:15, Biblia Habari Njema) Yesu Kristo alichangia furaha kwenye arusi fulani kwa kugeuza maji yawe “divai nzuri.”—Yohana 2:3-10.

Ni wazi kwamba Muumba anajua kabisa jinsi pombe inavyofanya kazi katika mwili na ubongo. Katika Biblia, Baba yetu wa mbinguni ‘anatufundisha ili tujifaidi wenyewe,’ na anatuonya kwa uzito tusinywe pombe kupita kiasi. (Isaya 48:17) Ona maonyo haya yaliyo wazi:

“Msiwe mkilewa divai, ambayo ina upotovu ndani yake.” (Waefeso 5:18) “Walevi . . . hawataurithi ufalme wa Mungu kamwe.” (1 Wakorintho 6:9-11, Jerusalem Bible) Neno la Mungu linashutumu “ulevi, ulafi na mambo mengine kama hayo.”—Wagalatia 5:19-21, BHN.

Sasa tuchunguze baadhi ya matokeo mabaya ya kunywa pombe kupita kiasi.

Matokeo Mabaya ya Kunywa Kupita Kiasi

Pombe inaweza kumnufaisha mtu kwa kadiri fulani, hata hivyo, inabadili sana jinsi akili na mwili unavyofanya kazi. Kunywa pombe kupita kiasi kunaweza kusababisha matatizo yafuatayo:

Akili ya mtu anayekunywa pombe kupita kiasi inaathiriwa hivi kwamba ‘hawezi kufikiri vizuri.’ (Methali 23:33, Today’s English Version) Allen aliyekuwa akinywa pombe kupita kiasi, ambaye anatajwa katika makala ya kwanza, anasema hivi: “Ulevi sugu si kasoro ya mwili tu; bali pia ni kasoro ya maoni na mtazamo wa mtu. Hajali jinsi anavyowaumiza watu wengine.”

Huenda mtu anayekunywa pombe kupita kiasi akashindwa kujizuia. Biblia inaonya hivi: “Divai na divai tamu ndivyo vinavyoondoa kusudi jema.” (Hosea 4:11) Jinsi gani? Tunapokunywa pombe huenda tukashindwa kuzuia mawazo na tamaa ambazo kwa kawaida tunazidhibiti, huenda hata tukaanza kuziona kuwa sawa na zenye kutamanika. Azimio letu la kufanya yaliyo sawa linaweza kudhoofika. Pombe inaweza kudhoofisha pia azimio letu la kudumisha mwenendo mzuri, na hivyo kusababisha madhara makubwa ya kiroho.

Kwa mfano, John aligombana na mke wake, akatoka kwa hasira, na kuingia katika baa. Alikuwa amekunywa kiasi fulani cha pombe ili apoe wakati mwanamke fulani alipomjia. Baada ya kunywa pombe zaidi, John alitoka pamoja na mwanamke huyo na akafanya uzinzi naye. Baadaye, John alijuta sana kufanya jambo ambalo hangefanya kamwe kama hangekuwa amekunywa pombe.

Mtu anayekunywa pombe kupita kiasi huenda akashindwa kudhibiti usemi na matendo. “Ni nani aliye na taabu sikuzote? Ni nani anayegombana na kupigana?” Biblia inajibu: “Kila mtu anayekaa mpaka usiku wa manane ili kuendelea kunywa.” (Methali 23:29, 30, Contemporary English Version) Mtu anayekunywa kupita kiasi anaweza kusikia kana kwamba “yuko baharini akiwa na kichefuchefu, na akining’inia juu ya mlingoti wa meli inayorushwa huku na huku baharini.” (Methali 23:34, TEV) Mwanamume ambaye amekunywa kupita kiasi huenda akaamka akiwa “na majeraha katika mwili mzima, hata asikumbuke jinsi alivyoumia.”—Methali 23:35, CEV.

Afya ya mtu anayekunywa kupita kiasi inaweza kuathiriwa. “Mwishowe [pombe] huuma kama nyoka; huchoma kama nyoka mwenye sumu.” (Methali 23:32, BHN) Wanasayansi wamethibitisha kwamba methali hiyo ya kale ni ya kweli. Pombe inaweza kumwathiri mtu kama sumu hatari kwa kusababisha kansa mbalimbali, uvimbe na magonjwa mengine ya ini, ugonjwa wa kongosho, kiwango cha chini cha sukari katika damu ya watu wanaougua kisukari, kiharusi, ugonjwa wa moyo, na pia inaweza kuathiri kijusi. Hayo ni kati ya matatizo mengi yanayoweza kumpata mtu anayekunywa pombe nyingi. Hata mtu anayekunywa pombe kupita kiasi mara moja tu anaweza kupoteza fahamu au kufa. Lakini madhara makubwa zaidi ya kunywa kupita kiasi hayatajwi katika vitabu vya tiba.

Madhara yaliyo makubwa zaidi. Mtu anayekunywa pombe nyingi anapatwa na madhara ya kiroho, hata kama hajalewa. Maneno haya ya Biblia ni wazi: “Ole wao wanaoamka asubuhi na mapema ili watafute tu kileo, wanaokawia mpaka giza la jioni sana hivi kwamba divai inawawasha!” Kwa nini? Isaya anaeleza madhara ya kiroho yanayotokana na kunywa kupita kiasi: “Hawauangalii utendaji wa Yehova, wala hawakuiona kazi ya mikono yake.”—Isaya 5:11, 12.

Neno la Mungu linatushauri tusiwe “kati ya watu wanaokunywa divai mno.(Methali 23:20) Wanawake wazee wanaonywa wasiwe “watumwa wa divai nyingi sana.” (Tito 2:3) Kwa nini? Pole kwa pole, bila kutambua, mtu anaanza kunywa pombe nyingi zaidi, mara nyingi zaidi. Hatimaye, yule anayekunywa huenda akafikiria sana pombe na kuwaza, ‘Asubuhi itafika wakati gani, ili niendelee kunywa?’ (Methali 23:35, CEV) Watu wanaokunywa pombe wako katika hali mbaya sana wanapotamani kunywa pombe asubuhi ili wapate nafuu baada ya kulewa usiku.

Biblia inaonya kwamba wale wanaokunywa “divai kupita kiasi,” au kushiriki katika “karamu za kupindukia, [na] mashindano ya kunywa . . . watatoa hesabu kwake yeye aliye tayari kuhukumu wale walio hai na wale walio wafu.” (1 Petro 4:3, 5) Naye Yesu alionya hivi kuhusu siku zetu zenye hatari: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku [ya Yehova] iwe juu yenu mara moja kama mtego.”—Luka 21:34, 35.

Basi, watu ambao wamezoea kunywa kupita kiasi wanaweza kufanya nini ili ‘wasilemewe na kunywa sana’?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Katika makala hii neno “pombe” limetumiwa kurejelea kileo, divai, na vinywaji vingine vinavyolevya.

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Zoea la kunywa pombe kupita kiasi linaweza kusababisha matatizo mengi