Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Watu Wanafanya Mambo Mabaya?

Kwa Nini Watu Wanafanya Mambo Mabaya?

Kwa Nini Watu Wanafanya Mambo Mabaya?

KUNA jambo moja ambalo karibu kila mtu anakubaliana nalo: Sisi sote si wakamilifu na hivyo tunafanya makosa na mambo ambayo tunajutia baadaye. Ingawa hivyo, je, hiyo ndiyo sababu watu wanatenda mambo mengi mabaya, yawe makubwa au madogo, ambayo tunajionea kwa macho yetu au kuyasikia karibu kila siku katika vyombo vya habari?

Ingawa wanadamu si wakamilifu, wanatambua kuwa kuna kanuni kuhusu mwenendo mzuri ambazo hazipaswi kuvunjwa, na kwamba wanadamu wana uwezo wa kuepuka kufanya maovu. Vilevile, watu wengi wanakubali kuwa kuna tofauti kati ya kusema jambo fulani lisilo la kweli bila kukusudia na kusema uwongo kimakusudi, na pia kuna tofauti kati ya kuwaumiza wengine bila kukusudia na kuua kimakusudi. Hata hivyo, mara nyingi mambo hayo ya kushtua hufanywa na watu wanaoonekana kuwa wa kawaida tu katika jamii. Kwa nini watu wanafanya mambo mabaya?

Biblia inaeleza mengi kuhusu jambo hilo. Inataja waziwazi sababu kuu zinazofanya watu watende mambo ambayo wanajua ni mabaya. Ona maoni ya Biblia kuhusu jambo hilo.

▪ “Uonevu mtupu unaweza kumfanya mtu mwenye hekima atende kiwazimu.”MHUBIRI 7:7.

Biblia inataja kuwa huenda hali fulani zikawafanya watu watende mambo ambayo kwa kawaida hawangefanya. Hata huenda wengine wakafanya mambo mabaya wakidhani kuwa kwa kufanya hivyo wataondoa hali ngumu na ukosefu wa haki. Kitabu Urban Terrorism kinasema hivi: “Mara nyingi, magaidi wengi hufanya mambo ya kigaidi kwa sababu ya kukatishwa tamaa na hali ngumu za kisiasa, kijamii, na kiuchumi.”

▪ “Kupenda sana fedha ni chanzo cha uovu wote.”1 TIMOTHEO 6:10, BIBLIA HABARI NJEMA.

Watu wengine husema kuwa hata watu wazuri wanaweza kutenda isivyofaa ikiwa wamepewa pesa. Watu ambao wanaonekana kuwa wenye urafiki na wema, huenda wakabadili utu wao na kuwa watu wabaya na wasio na urafiki kunapokuwa na uwezekano wa kupata au kupoteza pesa. Fikiria matendo mengine ya kuvunja sheria yanayosababishwa na pupa kama vile kuwatisha wengine ili kupata pesa, upunjaji, udanganyifu, utekaji nyara, na hata mauaji.

▪ “Kwa maana hukumu juu ya kazi mbaya haikutekelezwa upesi, ndiyo sababu moyo wa wana wa binadamu umeazimia kabisa ndani yao kutenda yaliyo mabaya.”MHUBIRI 8:11.

Andiko hilo linaonyesha waziwazi tabia ya wanadamu ya kufikiri kwamba wanaweza kufanya lolote ikiwa sheria haitekelezwi. Hiyo ndiyo sababu watu wanaendesha magari mbio sana, wanaiba mitihani, wanaiba pesa za umma, na kufanya mambo mengine mabaya hata zaidi. Ikiwa sheria haitekelezwi au ikiwa hakuna hofu ya kushikwa, huenda watu ambao kwa kawaida hufuata sheria wakafikiri kwamba wana uhuru wa kufanya mambo ambayo hawangefanya. Gazeti Arguments and Facts linasema: “Inaonekana kuwa wahalifu wengi huachiliwa bila kuadhibiwa, na hilo huwatia moyo raia wa kawaida kufanya uhalifu wa kinyama hata zaidi.”

▪ “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi.”YAKOBO 1:14, 15.

Mwanadamu yeyote anaweza kuwaza mambo yasiyofaa. Kila siku tunapata vishawishi vingi vya kutenda mabaya. Katika nyakati za Biblia Wakristo walishauriwa hivi: “Hakuna jaribu ambalo limewapata ninyi ila lile lililo kawaida kwa watu.” (1 Wakorintho 10:13) Hata hivyo, matendo yetu hutegemea uamuzi tunaofanya, yaani, tunaweza kuamua kutofikiri kuhusu mambo yasiyofaa au kuendelea kuyafikiria na kuyaruhusu yakomae akilini mwetu. Andiko lililotajwa ambalo linatoka katika barua ya Yakobo iliyoongozwa na roho ya Mungu, linatuonya kuwa ikiwa tutaruhusu tamaa mbaya “itunge mimba,” ni wazi kwamba matendo mabaya yatafuata.

▪ “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.”METHALI 13:20.

Rafiki zetu wanaweza kutuathiri sana—kwa njia mbaya au nzuri. Kwa hiyo, mara nyingi watu hutenda mambo bila kukusudia kwa sababu ya kulazimishwa na marafiki au, kama vile wengi wasemavyo, kwa sababu ya kushirikiana na watu wabaya, na hivyo kukumbwa na matatizo. Katika Biblia, neno “wajinga” linamaanisha watu wanaokataa kufuata mashauri yenye hekima ya Neno la Mungu, bali si watu wasio na akili. Iwe sisi ni wazee au vijana, ikiwa hatutachagua kwa busara marafiki na watu tunaoshirikiana nao, yaani, kwa kutegemea kanuni zinazofaa kutoka katika Biblia, basi tunaweza kutarajia ‘kupatwa na mabaya.’

Mistari hiyo ya Biblia iliyotajwa hapo juu na mingineyo inaeleza waziwazi kwa nini watu wa kawaida wanatenda mambo mabaya na yenye kuogopesha. Ingawa inafaa kuelewa kwa nini watu wanatenda mambo mabaya na yenye kushtua, je, kuna tumaini lolote kuwa hali zitabadilika? Ndiyo, kwa kuwa Biblia inaeleza sababu inayowafanya watu watende mambo mabaya na pia inaahidi kuwa mambo hayo hayatakuwapo tena. Ni ahadi gani hizo? Je, kweli mambo yote mabaya ulimwenguni yataisha? Habari inayofuata itajibu maswali hayo.