Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MKARIBIE MUNGU

“Ni Amri Gani Iliyo ya Kwanza Kati ya Zote? ”

“Ni Amri Gani Iliyo ya Kwanza Kati ya Zote? ”

Mungu anataka tufanye nini? Je, kuna sheria nyingi sana ambazo tunapaswa kufuata? Hapana. Kulingana na Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, yale ambayo Mungu anataka tufanye yanaweza kufafanuliwa kwa neno moja tu!—Soma Marko 12:28-31.

Kwanza fikiria wakati ambapo Yesu aliyasema maneno hayo. Alikuwa akifundisha hekaluni siku ya Nisani 11, siku chache tu kabla ya kifo chake. Adui zake walijaribu kumnasa kwa kumuuliza maswali ya kumtega. Kila mara, aliwanyamazisha kwa majibu yake. Kisha wakamuuliza Yesu hivi: “Ni amri gani iliyo ya kwanza kati ya zote?”—Mstari wa 28.

Hilo lilikuwa swali gumu. Baadhi ya Wayahudi walikuwa wamebishana kuhusu sheria iliyokuwa muhimu kabisa kati ya sheria zaidi ya 600 zilizofanyiza Sheria ya Musa. Wengine waliona kwamba sheria zote zilikuwa muhimu na kwamba lilikuwa kosa kuona sheria moja kuwa muhimu zaidi. Yesu angejibuje?

Katika jibu lake, Yesu hakutaja amri moja badala yake alitaja mbili. Kwanza alisema: “Nawe lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Mstari wa 30; Kumbukumbu la Torati 6:5) Maneno “moyo,” “akili,” “nafsi,” na “nguvu” yanakazia jambo moja. * Maana yake ni: Tunapaswa kumpenda Yehova kikamili, na kwa uwezo wetu wote. Kitabu kimoja cha marejezo kinasema hivi: “Mungu anapaswa kupendwa kabisa na kikamili.” Ikiwa unampenda Mungu, kila siku utajitahidi uwezavyo kuishi katika njia ambayo itampendeza.—1 Yohana 5:3.

Pili, Yesu alisema: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mstari wa 31; Mambo ya Walawi 19:18) Hatuwezi kumpenda Mungu na kumchukia jirani. Amri ya pili inatokana na ile ya kwanza. (1 Yohana 4:20, 21) Ikiwa tunawapenda majirani kama tunavyojipenda, tutawatendea kwa njia ambayo tungependa watutendee. (Mathayo 7:12) Na hivyo, kuonyesha kwamba tunampenda Mungu aliyetuumba sisi na pia majirani zetu, kwa mfano wake.—Mwanzo 1:26.

Mambo ambayo Yehova anataka waabudu wake wafanye yanaweza kufafanuliwa kwa neno moja tu: upendo

Amri ya kumpenda Mungu na jirani ni muhimu kadiri gani? “Hakuna amri nyingine yoyote iliyo kubwa kuliko hizi,” akasema Yesu. (Mstari wa 31) Katika simulizi linalofanana na hilo, Yesu alisema kwamba amri nyingine zote hutegemea amri hizo mbili.—Mathayo 22:40.

Si vigumu kumpendeza Mungu. Mambo anayotaka waabudu wake wafanye yanaweza kufafanuliwa kwa neno moja tu: upendo. Sikuzote upendo umekuwa—na utaendelea kuwa—alama inayotambulisha ibada ya kweli. Lakini upendo hauhusishi tu maneno na hisia; unapaswa kuonyeshwa kupitia matendo. (1 Yohana 3:18) Kwa nini usijifunze jinsi unavyoweza kusitawisha na kuonyesha upendo wako kwa Yehova, Mungu ambaye “ni upendo”?—1 Yohana 4:8.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Machi

Marko 9-16Luka 1-6

^ fu. 6 Katika Biblia neno “nafsi” hurejezea mtu kwa ujumla. Kwa hiyo “nafsi” inaweza kutia ndani “moyo,” “akili,” na “nguvu.”