Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Mungu Ana Maoni Gani Kuhusu Vita?

Mungu Ana Maoni Gani Kuhusu Vita?

Ungejibuje swali hilo? Wengi hufikiri kwamba Mungu huunga mkono vita. Wanasema kwamba aliwaamuru baadhi ya watumishi wake wa zamani wapigane vita; Biblia inathibitisha jambo hilo. Hata hivyo, wengine wanajua kwamba Yesu, Mwana wa Mungu, aliwafundisha wafuasi wake wawapende adui zao. (Mathayo 5: 43, 44) Kwa hiyo wanadai kwamba maoni ya Mungu kuhusu vita yamebadilika na sasa anachukia vita.

Unaonaje? Je, Mungu anaunga mkono vita? Ikiwa ni hivyo, anaunga mkono upande gani katika mizozano inayoendelea ulimwenguni? Majibu ya maswali hayo yatakusaidia uchunguze maoni yako kuhusu vita. Kwa mfano, ukijua kwamba Mungu anapenda vita na anaunga mkono upande unaopenda katika vita, huenda ukahisi vizuri na ukawa na uhakika kwamba mtashinda. Kwa upande mwingine, ungehisije ukijua kwamba Mungu anaunga mkono wapinzani wenu? Huenda ungefikiria kwa makini kuhusu msimamo wako.

Kuna jambo muhimu la kuzingatia. Kujua maoni ya Mungu kuhusu vita huenda kukabadili maoni yako kumhusu Mungu. Ikiwa wewe ni miongoni mwa watu wengi ambao wameteseka kwa sababu ya vita, huenda ungependa kupata jibu la swali, Je, Mungu anachochea watu wapigane ili wengine wateseke, au labda anakaa tu na hawajali wale wanaokandamizwa?

Huenda ukashangaa kujifunza kwamba jibu la Biblia linatofautiana sana na maoni hayo. Isitoshe, tangu zamani mpaka sasa maoni ya Mungu kuhusu vita hayajabadilika. Acheni tuone Biblia inasema nini kuhusu jinsi Mungu alivyoona vita katika nyakati za kale na katika karne ya kwanza Yesu alipokuwa duniani. Jambo hilo litatusaidia tujue jinsi Mungu anavyoona vita leo na ikiwa vita vitakwisha.