Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Angalia Ndege kwa Uangalifu

Angalia Ndege kwa Uangalifu

NDEGE wanaishi mahali pote katika dunia, na wako kati ya viumbe ambavyo ni rahisi kuangalia. Pia, umbo, rangi, nyimbo, na tabia mbalimbali za ndege zinaweza kufanya kipindi cha kuangalia ndege kiwe chenye kufurahisha kabisa.

Unaweza hata kuangalia ndege ukiwa nyumbani kwako. Kwa mufano, ndege anayeishi Ulaya anayeitwa blackbird akichimba ili kutafuta wadudu, ndege mukali mushika-nzi akinasa vidudu, hua dume akimutongoza hua dike, mbayuwayu akijenga kwa bidii nyumba yake, ao chiriku-­zahabu akilisha vitoto vyake vyenye njaa.

Ndege fulani watakushangaza wakati wanaruka katika anga ili kuwanasa wadudu; kwa mufano tai, kozi-kipanga, na vibombobombo. Wengine wanaweza kukufurahisha: shore wanaopigania chakula fulani, njiwa ya kiume anayevimbisha sehemu ya mbele ya mwili wake ili kumuvutia ndege dike ambaye anaonekana hamujali, ao mulio wa kikundi cha gala-waridi na gala-kijivu wakininginia, vichwa chini na miguu juu kwenye waya ya umeme kwa sababu ya kushindwa kusimama sawasawa. Utaona mambo mengine yenye kushangaza, kwa mufano, korongo wanaohamia mahali pengine wakipita juu sana, korongo wenye kibwenzi, ao bata-bukini. Ni wazi kwamba, kwa muda wa  miaka mingi sana watu wameona ndege wakihamia mahali pengine, watu wanaoangalia ndege hao wanashangazwa sana na uwezo wao wa kuenda safari ndefu sana wakiheshimu wakati ambao wanazoea kuhama. Kwa kweli, Muumbaji yeye mwenyewe alisema: ‘Korongo juu mbinguni anajua vema nyakati zake zilizowekwa; na njiwa-tetere na barawai na teleka wanaangalia vema wakati wa kila mumoja wao kuingia.’

Yeremia 8:7.

Ndege Katika Nyakati za Biblia

Biblia inazungumuzia mara nyingi ndege, zaidi sana ili kutufundisha mambo ya maana. Kwa mufano, kuhusu mbuni na uwezo wake wa kukimbia kwa mwendo wa haraka sana, Mungu alimuambia mwanaume mumoja anayeitwa Ayubu hivi: ‘Wakati anapopiga-piga mabawa yake juu, yeye humucheka farasi na mupandaji wake.’ * (Ayubu 39:13, 18) Pia, Mungu alimuuliza Ayubu hivi: ‘Je, ni kwa sababu ya uelewaji wako kwamba kipanga anapaa juu, . . . ao, je, ni kwa agizo lako kwamba tai anaruka kuelekea juu?’ (Ayubu 39:26, 27) Tunajifunza nini? Ndege wanatenda bila musaada wetu. Uwezo mbalimbali wa ndege unaonyesha hekima ya Mungu, si hekima yetu.

Mufalme Sulemani aliandika kuhusu “sauti ya njiwa-tetere,” ambaye anatangaza kuanza kwa majira ya kuchipua ao kuota tena kwa majani. (Wimbo wa Sulemani 2:12) Mutunga zaburi alitaja mbayuwayu alipoandika kuhusu tamaa yake ya kutumikia katika hekalu la Mungu. Akiwa na wivu kidogo, alisema: “Hata ndege amepata nyumba, na mbayuwayu amepata kiota chake, ambapo ameweka vifaranga vyake [karibu na] mazabahu yako kuu, Ee Yehova.”—Zaburi 84:1-3.

‘Baba yenu wa mbinguni anawalisha wao. Je, ninyi si bora kuliko wao?’—Mathayo 6:26

Kati ya maelezo mazuri zaidi kuhusu ndege, kuna yale yalitolewa na Yesu Kristo. Ona maneno haya yanayopatikana katika Mathayo 6:26: ‘Waangalieni kwa makini ndege wa mbinguni, kwa sababu hawapandi mbegu ao kuvuna ao kukusanya galani; na bado Baba yenu wa mbinguni anawalisha wao. Je, ninyi si bora kuliko wao?’ Mufano huo wenye kugusa moyo uliwahakikishia wafuasi wa Yesu kwamba wao ni watu wa maana machoni pa Mungu na kwamba hawapaswi hata kidogo kuhangaika kwa ajili ya kupata vitu vya lazima katika maisha.—Mathayo 6:31-33.

Leo, watu wengi sana wanafurahia kuangalia ndege—na hilo linaeleweka, kwa sababu tunashangazwa sana na tabia zao za kucheza-cheza, uzuri wao, njia zao za kutongozana, na nyimbo zao. Zaidi ya hilo, ndege wanaweza pia kufundisha wale wanaoziangalia kwa uangalifu mambo ya maana kuhusu maisha. Je, utaangalia ndege kwa uangalifu?

^ fu. 6 Mbuni ndiye ndege mukubwa zaidi na anayekimbia mbio sana kupita ndege wote; anapokimbia polepole anaweza kufanya kilometa karibu 72 kwa saa moja.